UBORESHAJI WA HUDUMA ZA AFYA MUSOMA VIJIJINI UNAENDELEA – KIJIJI CHA NYABAENGERE CHAANZA KUJENGA ZAHANATI YAKE

WANAVIJIJI wakisomba mawe kwa ajili ya ujenzi wa ZAHANATI ya Kijiji chao cha NYABAENGERE, Kata ya Musanja.

Na: Verediana Mgoma
Msaidizi wa Mbunge

WANAVIJIJI wa Jimbo la Musoma Vijijini kwa kushirikiana na SERIKALI, wameamua kujenga na kuboresha MIUNDOMBINU ya HUDUMA za AFYA ndani ya Vijiji vyao na Kata zao.

Mbunge wa Jimbo, Madiwani na Wazaliwa wa baadhi ya Vijiji wanachangia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu hiyo.

ZAHANATI ZILIZOPO NA ZINATOA HUDUMA

*Zahanati 24 za Serikali
*Zahanati 4 za Binafsi

ZAHANATI MPYA ZINAZOJENGWA

*Zahanati 14 zinajengwa

WODI ZA MAMA & MTOTO ZINAZOJENGWA

*Wodi 3 za Mama & Mtoto zinajengwa kwenye Zahanati za Bukima, Kisiwani Rukuba na Nyegina.

VITUO VYA AFYA VINAVYOTOA HUDUMA

*Vituo 2 vya Afya vya Murangi na Mugango vinatoa huduma.

*Zahanati ya Masinono inapanuliwa iwe Kituo cha Afya cha Kata hiyo ya Bugwema.

HOSPITALI YA WILAYA INAJENGWA

*Hospitali ya Wilaya inajengwa kwenye Kitongoji cha Kwikonero, Kijijini Suguti.

KIJIJI CHA NYABAENGERE CHAAMUA KUJENGA ZAHANATI YAKE

DIWANI wa Kata ya MUSANJA, Mhe Ernest Mwira amesema VIJIJI 3 vya Kata hiyo havina ZAHANATI hata moja na vyote vinahudumiwa na KITUO cha AFYA cha Kata jirani ya Murangi.

KIONGOZI huyo ameendelea kueleza kwamba baadhi ya WAGONJWA wanalazimika kutembea umbali wa zaidi ya KILOMITA 10 kwenda kupata matibabu kwenye Kituo hicho cha Afya.

Kwa hiyo, Kijiji cha NYABAENGERE kimeamua kujenga ZAHANATI yake ambayo imepangwa ikamilike ndani ya mwaka mmoja.

MTENDAJI wa Kijiji (VEO) cha Nyabaengere, Ndugu Emmanuel Eswaga amesema utekelezaji wa MPANGOKAZI wa Mradi huo, unamtaka KILA MWANAKIJIJI mwenye uwezo wa kufanya kazi, ATACHANGIE Tsh 24,000, na kila KITONGOJI kitasomba mawe, mchanga na maji.

MCHANGO WA DIWANI

Diwani, Mhe Ernest Mwira ataanza kutoa MICHANGO yake kwa kuchangia SARUJI MIFUKO 20

MCHANGO WA MBUNGE
WA JIMBO

Mbunge wa Jimbo, Prof Sospeter Muhongo, AMEKUBALI kuanza kuchangia ujenzi huo na ataanza kwa kuchangia SARUJI MIFUKO 100.

OMBI KWA WAZALIWA WA KATA YA MUSANJA

Zahanati inayoanza kujengwa Kijijini Nyabaengera itatoa HUDUMA za Afya kwa Vijiji jirani vya Mabui Merafuru na Musanja vyote vya Kata hiyo.

Kwa hiyo, WAZALIWA wa Kata ya MUSANJA wanaombwa wachangie MRADI huu kwa kutuma MICHANGO yao kwa DIWANI au VIONGOZI wengine wa Kata hiyo.

Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Musoma Vijijini
www.musomavijijini.or.tz