HAYUPO MWANAFUNZI WA KIDATO CHA KWANZA 2020 (wamechaguliwa 3,502) ATAKAYEBAKI NYUMBANI

Mbunge wa Jimbo (mwenye T-shirt nyeupe) akiwa na Wananchi wa Kata ya Bugoji wakipiga HARAMBEE ya kukamilisha ujenzi wa Vyoo vya Dan Mapigano Memorial Secondary School.

SEKONDARI 2 MPYA ZINAZOJENGWA JIMBONI ZAOMBA ZIFUNGULIWE TAREHE 13.1.2020
(1) Busambara Secondary School ya Kata ya Busambara (Vijiji vya Maneke, Kwikuba na Mwiringo).
Vyumba vipya 3 vya Madarasa na madawati 40 kila darasa viko tayari. Jengo la Ofisi za Walimu linakamilishwa kwa kuwekwa milango na madirisha. Ujenzi wa Vyoo vya Wasichana, Wavulana na Walimu UTAKAMILIKA Alhamisi, 9.1.2020.
KIKAO cha HARAMBEE cha Wananchi na Mbunge wao, Prof Sospeter Muhongo, cha tarehe 2.1.2020 kimetoa msukumo mkubwa wa ukamilishaji wa ujenzi huo.
Mbali ya MICHANGO ya awali ya Mbunge huyo, amekubali KUNUNUA RANGI ya kupaka ndani na nje ya Majengo 3 hayo ya Vyoo na Jengo la Ofisi za Walimu. Baadhi ya WAZALIWA wa Kata ya Busambara  WANAENDELEA KUCHANGIA ujenzi wa Sekondari ya Kata yao – AHSANTENI SANA!
Wananchi wa Vijiji 3 vya Kata ya Busambara wameandika barua wakiiomba Serikali iwaruhusu Sekondari yao IFUNGULIWE tarehe 13.1.2020 na KUCHUKUA Wanafunzi 142 ya Kata yao waliochaguliwa kujiunga na Kidato cha kwanza Januari 2020.
(2) Dan Mapigano Memorial Secondary School ya Kata ya Bugoji (Vijiji vya Kanderema, Kaburabura na Bugoji)
Vyumba vipya 5 vya Madarasa na madawati 40 ya kila darasa viko tayari. Ofisi za Walimu zimekamilika. Ujenzi wa VYOO vyote (wasichana, wavulana na walimu) vya shule utakamilika ifikapo Jumatano, 8.1.2020. Kwenye HARAMBEE ya ujenzi huu, Mbunge wao, mbali ya MICHANGO yake ya awali, amechangia tena utengenezaji wa MILANGO mipya 12 ya Vyoo hivyo. Baadhi ya WAZALIWA wa Kata ya Bugoji wamechangia ujenzi wa Sekondari ya Kata yao.
Vijiji 3 vya Kata ya Bugoji vimeiiomba Serikali iwaruhusu Sekondari yao ifunguliwe tarehe 13.1.2020 na KUCHUKUA WANAFUNZI 141 wa Kata hiyo waliochaguliwa kujiunga na Kidato cha Kwanza Januari 2020.
KUPUNGUZA MRUNDIKANO WA WANAFUNZI MADARASANI
Vyumba VIPYA vya Madarasa VIZIPOPATIKANA kwenye baadhi ya Sekondari patakuwepo na MRUNDIKANO MKUBWA wa Wanafunzi madarasani mwao:
Bugwema (vyumba vipya 3 vinahitajika), Bulinga (3), Kasoma (3), Nyakatende (2), Nyanja (1) na Rusoli (1).
Mbunge wa Jimbo, Prof Sospeter Muhongo ANAFANYA VIKAO VYA HARAMBEE vya kukamilisha ujenzi wa Vyumba VIPYA vinavyohitajika kwenye Sekondari hizo. Baadhi ya WAZALIWA wa Kata zenye upungufu wa Vyumba vya madarasa WANACHANGIA ujenzi huu.
Kwa hiyo, kwa Jimbo la Musoma Vijijini, HAYUPO Mwanafunzi wa Kidato cha kwanza 2020 (3,480 Sekondari za Kata na 22 za Bweni) ATAKAYEBAKI nyumbani kwa sababu ya UKOSEFU wa Vyumba vya Madarasa – muhimu ni kupatikana kwa Vyumba vipya ili kila darasa lichukue Wanafunzi wasiozidi 40.