PROF MUHONGO ATUNUKIWA HATI YA HESHIMA

Msaidizi wa Mbunge, Ndugu Fedson Masawa akipokea HATI ya HESHIMA kwa niaba ya Mbunge wa Jimbo Prof Muhongo. Mbunge wa Jimbo hakuwepo kwani alikuwa kwenye maziko ya Marehemu Mhe Balozi Paul James Ndobho.

Na: Fedson Masawa
Msaidizi wa Mbunge

JUMUIYA ya Wazazi Wilaya ya Musoma Vijijini leo September 14, 2019 imemtunuku HATI ya HESHIMA Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof Sospeter Muhongo.

Ndugu Julius Kambarage Masubo, Mjumbe wa Baraza la Wazazi Taifa kutoka Mkoa wa Mara ndiye aliyekuwa MGENI RASMI wa Baraza la Wazazi Wilaya ya Musoma Vijijini lililokutana leo Kijijini Chumwi

Akikabidhi HATI hiyo, MGENI RASMI amesema, “HATI hii ni Ishara ya kipekee ya kutambua Mchango na Utendaji kazi mzuri na uliotukuka wa Mbunge wa Jimbo katika kuitekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2015 – 2020 ndani ya Jimbo la Musoma Vijijini na Halmashauri ya Wilaya ya Musoma.

Mgeni Rasmi huyo aliendelea kusema kwamba, HATI hiyo ni kielelezo cha kutambua MCHANGO MKUBWA wa Mbunge huyo kwenye Chama (CCM) na Jumuiya zake zote.

Ndugu Kambarage Masubo ametoa pongezi nyingi kwa Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof Muhongo kwa Uongozi Shirikishi unaowaunganisha Wananchi wa Musoma Vijijini katika kuharakisa Maendeleo Jimboni mwao.

Jimbo hili halina malumbano ya kisiasa wala halina mivutano ya kikabila – Mbunge wa Jimbo wanawaunganisha Wananchi wote kwenye MIRADI ya Maendeleo bila ubaguzi wa aina yo yote ile.

Wengine waliotunukiwa HATI ya HESHIMA na Jumuiya ya Wazazi ni pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma, Mhe Charles Magoma Nyambita pamoja na Diwani wa Kata ya Bukima Mhe January Simula.

Ndugu Kambarage Masubo ameikumbusha Jumuiya ya Wazazi wawe kitu kimoja kuhakikisha Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatekelezwa kwa kasi kubwa chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt John Joseph Pombe Magufuli.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Musoma Vijijini, Ndugu Phares Maghubu amesisitiza kuwa Jumuiya ya Wazazi inaendelea kuimarisha mipango yao ya utunzaji wa Mazingira, kuhamasisha uboreshaji wa elimu na kuimarisha nidhamu na maadili kwa Vijana ili kuwa na kizazi chenye maadili mazuri na chenye kujituma katika shughuli za ki-uchumi na maendeleo.