WANAKIJIJI NA SERIKALI KUPITIA MRADI WA EQUIP  WAKAMILISHA UJENZI WA SHULE SHIKIZI MWIRINGO

Shule SHIKIZI Mwiringo ikiwa imekamilika na tayari kupokea Wanafunzi kutoka Kitongoji cha Ziwa na kwingineko Kijijini Mwiringo, Kata ya Busambara.

Jumanne, 09.07.2019
Na: Hamisa Gamba
Msaidizi wa Mbunge
Wananchi wa Kijiji cha MWIRINGO, Kata ya Busambara WAMESHIRIKIANA na SERIKALI yetu kupitia Mradi wake na Wafadhili wa EQUIP kufanikisha ujenzi wa Shule SHIKIZI Kijijini humo.
Shule hiyo imejengwa kwenye Kitongoji cha Ziwa ndani ya Kijiji cha Mwiringo.
Shule Shikizi Mwiringo ni kati ya SHULE KUMI (10)  MPYA za MSINGI zinazojengwa kwenye Jimbo la Musoma Vijijiji lenye Jumla ya Shule za Msingi 113 (111 za Serikali na 2 za Binafsi).
Ujenzi wa hizo Shule kumi (10) ukikamilika na baadae zikapanuliwa ili kuchukua Wanafunzi wa Darasa la I hadi VII, Jimbo letu litakuwa na Jumla ya Shule za Msingi 123 (121 za Serikali na 2 za Binafsi). Safari ya kuelekea kwenye SHULE ZA MSINGI MBILI (2) KWA KILA KIJIJI (Vijiji 68, Kata 21) inaenda vizuri!
EQUIP (The Education Quality Improvement Programme) ilitoa Shilingi MILIONI 60 kwa ajili ya ujenzi wa: (i) Vyumba viwili (2) vya Madarasa,  (ii) Ofisi moja (1) ya Walimu, na (iii) Matundu sita (6) ya Vyoo, yaani 4 ya Wanafunzi na 2 ya Walimu.
Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Mwiringo, Mwl Surusi Mnene ambae ndie Mlezi wa Shule hiyo SHIKIZI, alieleza kuwa ujenzi huo ulianza Januari 2019 na hadi hivi sasa ujenzi umekamilika. Matenki mawili (2) ya kuvuna MAJI yako tayari na Mafundi wanakamilisha MADAWATI 50.
Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mwiringo, Ndugu Coletha Felix alieleza kuwa amefurahishwa sana na Jitihada za Wananchi wa Kijiji cha Mwiringo kwa NGUVUKAZI zao na ushirikiano wao mkubwa waliouonesha katika kuhakikisha ujenzi huo unakamilika haraka. Wananchi hao wamejitolea kusomba mawe, kokoto, mchanga na maji kwa ajili ya ujenzi huu.
Wanakijiji cha Mwiringo na Viongozi wao wa Jimbo la Musoma Vijijini, kwa pamoja, wanaishukuru sana SERIKALI yetu kwa jitihada kubwa inazofanya kwa kuwaunga mkono kwenye MIRADI ya MAENDELEO ikiwemo Miradi ya ELIMU na AFYA Kijijini mwao.