ZAHANATI YA KIJIJI CHA MWIRINGO KUANZA KUTOA HUDUMA MWEZI UJAO

Mbunge wa Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo mapema leo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mwiringo (wengine hawapo pichani) mbele ya jengo la zahanati ya Mwiringo ambayo itaanza kutoa huduma za afya Machi, 1, 2018.

Na. Mwandishi Wetu

WAKAZI wa Kijiji cha Mwiringo, Halmashauri ya Musoma vijijini na Mbunge Prof. Sospeter Muhongo, wamekubaliana huduma za matibabu kwenye zahanati ya kijiji hicho zianze kutolewa Machi, 1, mwaka huu.

Uamuzi huo umefikiwa kwenye mkutano uliofanyika kwenye kijiji cha Mwiringo, Kata ya Busambara ambapo Prof. Muhongo amechangia  meza, viti na vifaa vingine vinavyohitajika ili kuharakisha ufunguzi wa zahanati hiyo.

Wiki chache zilizopita, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Musoma Dkt. Makwanda alisema, jambo linalochelewesha zahanati hiyo kuanza kutoa huduma, ni ukosefu wa meza nne na viti nane na vifaa vingine, hivyo kwa mchango huo wa mbunge kero ya muda mrefu ya wananchi wa kijiji cha Mwiringo ya kukosa huduma za afya inaelekea kupata ufumbuzi.

Zahanati hiyo ilianza kujengwa Mwaka 2011 kwa nguvu za wananchi na kwa mchango mkubwa wa vijana wasomi na wataalamu kutoka Kijiji cha Mwiringo, ujenzi wake ulikamilika mwaka 2014 na awali zahanati hiyo ilipangwa ianze kutoa huduma Mei, 1, 2018, lakini kutokana na hamasa iliyopo, itaanza kutoa huduma mwezi ujao.