VIJANA WAHIMIZWA KUONYESHA VIPAJI VYAO KATIKA SOKA

Msaidizi wa Mbunge Fedson Masawa akimpongeza nahodha wa timu ya Zahanati Mafuru Majogoro (kushoto) na kumkabidhi zawadi yao ya mbuzi watatu baada ya kuibuka mabingwa wa Ligi ya ‘Bashiri Vitongoji Ndondo Cup Bukima.’

Na Mwandishi Wetu

VIJANA wametakiwa kujitokeza kwa wingi na kuonyesha vipaji vyao katika mchezo wa mpira wa miguu na hatimaye kutumia vipaji hivyo kujiajiri kupitia timu kubwa za ndani na nje ya Jimbo la Musoma vijijini.

Hayo yamesemwa na msaidizi wa Mbunge Fedson Masawa aliyekuwa mgeni rasmi katika fainali za Ligi ya vitongoji vya kijiji cha Bukima maarufu kama “Bashiri Vitongoji Ndondo Cup Bukima,” iliyoshirikisha timu kutoka vitongoji nane, ikiwa ni maandalizi ya ligi kubwa inayotarajiwa kuanza hivi karibuni kwenye kata ya Bukima.

Masawa alisema, kufanyika kwa mashindano hayo ni hatua nzuri ya kufungua njia kwa vijana wa Musoma vijijini katika kutumia vizuri  vipaji vyao na kumpongeza muandaaji wa mashindano hayo Bashiri Chirwa kwa jitihada anazofanya katika kuhamasisha mpira wa miguu kwenye kata hiyo.

Katika mashindano hayo, timu ya Zahanati ilichukua nafasi ya kwanza kwa kushinda magoli 2 dhidi ya Senta iliyopata goli 1 na kushika nafasi ya pili ambapo mshindi wa kwanza alipata zawadi ya mbuzi watatu na mshindi wa pili alipata mbuzi wawili.