MAADHIMISHO YA MIAKA 41 YA CCM YAPAMBA MOTO BUGWEMA

Baadhi ya akinamama wakiimba wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 41 ya kuzaliwa CCM yaliyofanyika kwenye kijiji cha Bugwema

Na. Mwandishi Wetu

DIWANI wa Kata ya Bugwema Ernest Maghembe amesema, Chama cha Mapinduzi (CCM) kimefanya mageuzi makubwa kwa kipindi ilichokaa madarakani.

Akizungumza kwenye sherehe za maadhimisho ya miaka 41 tangu kuzaliwa CCM yaliyofanyika kwenye kijiji cha Bugwema, diwani Maghembe alisema, CCM imefanya mageuzi makubwa ambayo wanachama wake wanapaswa kujivunia hususani kwenye elimu, afya, na kilimo.

Aidha, diwani Maghembe alitumia fursa hiyo kutoa pole kwa familia na watanzania wote kufuatia msiba wa mmoja wa waasisi wa chama hicho Mzee Kingunge Ngombale Mwiru aliyefariki wiki iliyopita na kuzikwa leo jijini Dar es Salaam.

“Tutakumbuka mchango wa mzee Kingunge kwa nchi yetu na chama, tutamuenzi kwa uzalendo wake” alisema diwani Maghembe.

Kwa upande wake msaidizi wa mbunge Hamisa Gamba aliwaomba wanachama wa CCM kuachana na makundi yanayoweza kuleta mgawanyiko ndani ya chama na badala yake maadhimisho hayo yatumike kuwajenga kifikra na katika uwajibikaji hasa kwenye kilimo, elimu na afya.

Msaidizi huyo pia aliwataka wanachama wa CCM na wananchi wote kujiandaa kwa kilimo cha alizeti na ufuta kwa kuwa mbegu zinatolewa bure na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini huku akisisitiza uwepo wa soko la uhakika kwenye mazao hayo.

Sherehe hizo ziliadhimishwa kwa michezo mbalimbali ya vijana ikiwemo kwaya na mpira wa mguu kutoka kwa timu zilizopo kwenye kata hiyo.