WANANCHI NYASAUNGU WAFICHUA SIRI YA MAFANIKIO YAO

Wananchi wa kijiji cha Nyasaungu waliojitolea kushiriki ujenzi wa zahanati ya kijiji chao wakiwa kwenye picha ya pamoja.

Na. Fedson Masawa

WANANCHI wa kijiji cha Nyasaungu wamesema siri ya maendeleo kijijini hapo ni umoja, mshikamano na kuheshimiana baina ya wananchi na viongozi ambao kwa kiasi kikubwa ndio wanahusika kusimamia shughuli hizo.

Wananchi hao walisema, maendeleo ni kuwa na mipango ya pamoja, kusikilizana na kuwajibika katika kuchangia shughuli yoyote ya maendeleo bila kusukumwa, hali ambayo inawapa moyo wafadhili mbalimbali na kuungana nao ili kuwapatia huduma bora kijijini hapo.

Katika hatua nyingine, wananchi hao wameishukuru Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini kwa namna ambavyo imewarudisha katika utaratibu wa maendeleo kupitia hamasa na kuwapa moyo wa matumaini ili kufanikisha ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Nyasaungu.

Naye Kaimu Mtendaji wa kijiji hicho  Janas Itembe alisema, baada ya kukamilika kwa maandalizi ya kukusanya kokoto na mchanga, shughuli rasmi ya kurekebisha msingi wa zahanati itaanza Februari 5, 2018 baada ya mhandisi wa wilaya kufika kwa ajili ya maelekezo.