PROF. MUHONGO ACHANGIA MATIBABU YA MPIGA KURA WAKE

Msaidizi wa Mbunge, Fedson Masawa (wa pili kushoto) akimkabidhi Muriti Mafuru fedha taslimu shilingi 300,000 ambayo ni ahadi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ili kufanikisha huduma ya matibabu ya Mzee Mafuru anayesumbuliwa na tatizo la kibofu cha mkojo na tatizo la mguu.

Na Mwandishi Wetu

MSAIDIZI wa Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Fedson Masawa amekabidhi kiasi cha fedha za matibabu kwa familia ya Mzee Mafuru Kati ambaye anasumbuliwa na matatizo ya mguu na kibofu cha mkojo.

Wakati alipotembelea kijiji cha Busekera kuangalia madhara yaliyotokana na mafuriko yaliyovikumba vijiji vingi jimboni humo, Prof. Sospeter Muhongo aliahidi kumsaidia mzee huyo shilingi 300,000 kwa ajili ya matibabu.

Akikabidhi fedha hizo, Masawa aliwataka wanafamilia wanaomuuguza mzee huyo kuwa na uvumilivu na kujituma katika kuendelea kumuhudumia Mzee Mafuru ambaye ni mkuu wa kaya hiyo.

“Ndugu zangu mbunge ametimiza ahadi yake aliyoiahidi. Kuuguza ni kazi ngumu, kinachotakiwa kwenu ni kuwa na moyo wa uvumilivu na kujituma ili kurejesha afya ya mzee wetu” alisema Masawa.

Akizungumza kwa niaba ya familia hiyo, mmoja wa watoto wa mzee huyo Muriti Mafuru alimshukuru Prof. Sospeter Muhongo kwa kuungana na familia yao ili kuhakikisha afya ya mzee wao inaimarika.

Muriti aliongeza kuwa, watajitahidi kutumia fedha hizo katika kufanikisha matibabu ya mzee wao na si kwa matumizi tofauti.

“Tunamshukuru Prof. Muhongo kwa kuungana nasi kwa mchango wake ili kuimarisha afya ya mzee wetu, mwenyezi Mungu ambariki sana Mbunge. Pia tutajitahidi kutumia fedha hizi kwenye matibabu wala siyo kazi nyingine” aliahidi kijana huyo.