MBUNGE MUSOMA VIJIJINI AIWEZESHA FAMILIA KUPITIA KILIMO

Msaidizi wa Mbunge Fedson Masawa (kulia) akikagua shamba la mke wa mzee Kocha baada ya kukamilika kulimwa. Kushoto ni Buinda Kocha ambaye analimiwa shamba hilo akiwa na Chikopa Manumbu (katikati) ni mmoja wa vibarua waliokuwa wakilima shamba hilo.

Na. Mwandishi Wetu

HATUA ya awali ya ulimaji wa shamba la marehemu mzee Kocha aliyekuwa mkazi wa kijiji cha Busekera imekamilika na wakati wowote zoezi la upandaji wa mbegu litafanyika.

Shamba hilo lenye ukubwa wa heka nne, limeandaliwa kwa ajili ya kusaidia familia ambayo imeachwa na mzee huyo ili ijimudu kiuchumi na chakula.

Wakati wa ziara yake kwenye kijiji cha Busekera, Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo alitembelea familia hiyo kutoa pole baada ya kupatwa na msiba ambapo mke wa marehemu mzee Kocha alielezea ugumu wa maisha unaoikabili familia yake na kuomba msaada wa mbunge.

Kutokana na ombi hilo, Prof. Muhongo alitoa ushauri wa kulima shamba hilo na kupanda mahindi na mtama ili familia hiyo ipate chakula na kuuza mazao ya ziada na kujipatia fedha za kukidhi mahitaji mengine muhimu.

Msaidizi wa mbunge Fedson Masawa, akikagua maendeleo ya shamba hilo alisema, wakati wowote wanaweza kuanza kupanda mbegu kuwahi mvua zilizoanza kunyesha ili kwa siku za usoni familia hiyo iweze kujikwamua kutokana na hali ngumu ya kiuchumi.

“Wakati wowote tutaanza kupanda mbegu ili tuwahi mvua ambazo zimeanza kunyesha na mbunge ameahidi kutoa gharama zote za ulimaji pamoja na kununua mbegu” alisema Masawa.