MBUNGE MUSOMA VIJIJINI ATIMIZA AHADI YAKE KIJIJI CHA SEKA

Diwani wa kata ya Nyamrandirira Ruteli Maregesi (aliyesimama kushoto) na msaidizi wa mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Verdiana Mgoma (wa kwanza kulia), wakikabidhi misaada ambayo iliahidiwa na mbunge Prof. Sospeter Muhongo kwa familia ya Nyambita Nyambea wakazi wa kijiji cha seka. 

Na. Mwandishi Wetu

MBUNGE wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ameendelea kutimiza ahadi ya kuzisaidia familia zilizoomba msaada kufuatia maafa yaliyotokea hivi karibuni kwenye maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.

Wakati wa ziara yake, baadhi ya wahanga akiwemo Nyambita Nyambea mkazi wa Seka, alimuomba mbunge amsaidie kulipa kodi ya nyumba ili aishi na familia yake kwa kipindi ambacho atakuwa kwenye maandalizi ya kujenga makazi mapya.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa msaada huo na msaidizi wa mbunge Verdiana Mgoma, Nyambita alimshukuru Prof. Muhongo kwa msaada wake na kumuomba aendelee na moyo huo wa kujitolea kwa watu wasiojiweza.

“Mbunge aliahidi kunilipia kodi ya nyumba kwa muda wa miezi sita baada ya nyumba yangu kuanguka kutokana na mvua iliyoambatana na upepo mkali, hivi leo nimepokea kiasi cha shilingi 84,000 ambayo ni kodi ya miezi sita, hivyo kupitia msaada huu, hadi kipindi cha kodi kuisha nitakuwa nimepata nguvu za kuanza ujenzi na kurudi kwenye nyumba yangu kama awali” alisema Nyambita.

Aidha Nyambita aliongeza kuwa, mbunge alitoa ahadi ya kumnunulia mwanae Nyafuru viatu vya shule, tayari amepokea jozi mbili za viatu kwa ajili ya masomo na mtoto huyo ameahidi kufanya vizuri zaidi katika masomo yake.

Kwa upande wake diwani wa kata ya Nyamrandirira Ruteli Maregesi ambaye alishuhudia makabidhiano hayo, alimshukuru Prof. Muhongo kwa dhamira na nia ambayo ameonyesha kwa wananchi wake hasa kuwa na moyo wa kujitolea, huku akikiri kwamba kwa muda aliofanya naye kazi amejifunza mambo mengi.

“Kwa niaba ya wakazi wa kata ya Nyamrandirira tunatoa shukrani zetu na kumuombea kheri” alisema diwani Maregesi.