TATHIMINI YA ATHARI ZA MAFURIKO YAANZA MUSOMA VIJIJINI

Baadhi ya kaya zilizopata maafa kutokana na kimbunga zikichukuliwa tathimini mpya kwa ajili ya maandalizi ya ripoti kamili ya Jimbo zima la Musoma vijijini. Pichani ni Mtendaji wa kijiji cha Bukumi Fred Jeremia ambaye ameambatana na ofisi ya Mbunge kuchukuwa tathimini ya uharibifu huo.

Na Mwandishi Wetu

SIKU chache baada ya Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kuagiza wasaidizi wake kwa kushirikiana na viongozi wengine kuanza kupitia upya tathimini ya uharibifu uliosababishwa na kimbunga na mafuriko, tayari zoezi hilo limeanza.

Wasaidizi wa mbunge na watendaji mbalimbali wa kata na vijiji wameanza kupitia upya takwimu halisi ya maafa hayo katika maeneo ya jimbo la Musoma vijijini ambapo baada ya tathimini hiyo, ripoti kamili ya maafa itaandaliwa kwa ajili ya kuiwasilisha katika mamlaka husika.

Zoezi hilo lilianza 27, Novemba mwaka huu linatarajiwa kukamilika mapema wiki hii ambapo ripoti hiyo itajumuisha hali halisi ya uharibifu uliotokea katika kaya husika, uharibifu uliosababishwa na mafuriko katika mashamba mbalimbali kwa kanda zote za Majita, Mugango na Bukwaya pamoja na ramani halisi ya jimbo inayoonesha maeneo husika yalipotokea maafa hayo.

Ili kufanikisha zoezi hilo kwa haraka zaidi, ofisi ya Mbunge imewaomba wananchi na viongozi wa kata na vijiji husika ambao pia ni waathirika wa matukio hayo kutoa ushirikiano wa hali ya juu ili kuharakisha ripoti hiyo.