KILIMO CHA MPUNGA CHATOA FURSA NYINGINE KWA WANANCHI MUSOMA VIJIJINI

Mmoja wa wakulima wa mpunga Amina Masatu akihamisha mbegu kutoka kwenye kitalu kupeleka kwenye majaruba tayari kwaajili ya kupandwa.

Na. Verdiana Mgoma

IDADI ya wakulima wanaojitokeza kulima mpunga kwa kutumia njia ya umwagiliaji inaongezeka kutokana na hamasa inayoendelea kutolewa na wataalamu mbalimbali wa kilimo na viongozi wa serikali.

Afisa kilimo wa kata ya Suguti Masinde Mjarifu alisema, awali haikuwa kazi rahisi kuwashawishi wananchi kulima mpunga kwa kuhofia uhaba wa mvua, lakini baada ya kuelimishwa kuhusu kilimo cha umwagiliaji, wengi wamejitokeza kulima huku wakiwa na matumaini ya kufanikiwa kupitia kilimo hicho.

“Mbali na kuwahimiza kulima kwa umwagiliaji, pia tunawahimiza kutumia mbegu za mpunga wa nchi kavu, fursa hii ya mbegu za mpunga wa nchi kavu ni fursa kwa wakulima wengi zaidi kuzalisha mpunga bila kulazimika kuhitaji maeneo yaliyozoeleka ya mabondeni” alisema Mjarifu.

Mmoja wa wakulima wa mpunga kijijini Suguti, Amina Masatu alisema, wameamua kuanzisha mashamba darasa yatakayowasaidia hasa upande wa kilimo, lengo ni kutambulisha kilimo cha umwagiliaji kwa mazao ya nafaka; mpunga wa nchi kavu.

“Kuwepo kwa mashamba darasa ni kufundisha vikundi mama ili kueneza elimu inayopatikana kwa malengo ya kuwepo kwa wakulima wengi kwenye kilimo cha umwagiliaji” alisema.

Aidha, mkulima huyo aliongeza: “Kilimo hiki cha mpunga kina hamasa kubwa kwetu, lakini changamoto tunazo kumbana nazo ni pamoja na upatikanaji wa elimu bora ya kilimo cha mpunga cha nchi kavu, kutokuwepo kwa wafadhili watakao saidia kutoa mbegu, upatikanaji wa mbolea bora itakayo saidia katika ukuaji na masoko kwaajili ya kuuzia mazao yao endapo kutakuwepo msaada wa kutatua changamoto hizo tuna imani kilimo kwetu kitakuwa ni fursa ya pekee.”