BUSAMBA WAFANIKISHA UJENZI WA CHOO CHA WATUMISHI NA MAKTABA

Mafundi wakiendelea na shughuli za ujenzi wa choo cha walimu katika shule ya msingi Busamba ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa matumizi ya mifuko 60 ya saruji iliyotolewa na Mbunge wa Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo shuleni hapo. Kulia ni Maisha Tengeja, mwalimu wa shule ya msingi Busamba.

Na. Ramadhani Juma

SERIKALI ya kijiji cha Busamba wamefanikisha ujenzi wa choo cha walimu katika shule ya msingi Busamba iliyopo kata ya Nyegina, jimbo la Musoma vijijini.

Ujenzi huo unafuatia baada ya kijiji hicho kufanya maamuzi ya kujenga maktaba ya shule hiyo kwa kutumia mchango wa mifuko 60 ya saruji iliyotolewa na Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo na upo kwenye hatua nzuri.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Mwalimu wa taaluma wa shule ya msingi Busamba Anna Mweya kwa niaba ya mkuu wa shule hiyo alisema, mifuko 60 iliyotolewa na Mbunge ilifanya kazi ya ujenzi wa maktaba, maamuzi ambayo yalilenga kuboresha mazingira ya kutunzia vitabu pamoja na wanafunzi kujisomea.

Anna aliongeza kuwa, baada ya kukamilisha ujenzi huo, serikali ya kijiji iliamua kujenga choo cha walimu kwa kutumia matofali yaliyosalia ikiwa ni njia pekee ya kumaliza changamoto hiyo shuleni hapo.

Mwalimu Anna aliendelea kufafanua, maamuzi ya kujenga maktaba na choo cha walimu hakumaanishi kuwa shule ya Busamba haina upungufu wa vyumba vya madarasa, bali ni katika kuimarisha mazingira ya utoaji wa huduma ya elimu.

Alisema, kwa wastani shule ya Busamba ina jumla ya wanafunzi 1,025 na ina upungufu wa vyumba 18 na vilivyopo ni vyumba 10 tu, hivyo serikali ya kijiji hicho imekamilisha ujenzi wa chumba kimoja cha darasa na kimeshaezekwa.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Busamba Kadenge Maanya amethibitisha matumizi ya mifuko hiyo 60 ya saruji katika ujenzi wa maktaba na choo cha walimu ikiwa ni sehemu ya mahitaji makubwa ya shule yao kwa wakati huu.

Mwenyekiti huyo pia alisema, mbali na ujenzi wa maktaba na choo cha walimu, wananchi wa Busamba kwa kushirikiana na serikali yao wamekamilisha ujenzi wa chumba kimoja cha darasa.