MCHANGO WA MBUNGE WAFANIKISHA UEZEKAJI WA NYUMBA YA MWALIMU

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Bukumi (katikati) akiwa na mafundi wakati wa uezekaji wa nyumba ya mwalimu katika shule ya msingi Bukumi.

 

Na. Fedson Masawa

MCHANGO wa mabati 100 yaliyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo katika shule ya msingi Bukumi, umefanikisha zoezi la uezekaji wa nyumba ya mwalimu mkuu katika shule hiyo.

Mwenyekiti wa kijiji cha Bukumi Nyaonge Maligo amemshukuru Prof Muhongo kwa mchango mkubwa alioutoa kijijini hapo kwa kuwa umewasaidia kupiga hatua nzuri ya maendeleo na wananchi wake kuwajibika kwa sehemu ndogo ya kukamilisha ujenzi huo.

“Kwa niaba ya wananchi wangu, namshukuru sana Prof. Muhongo kwa mchango huu, tumepiga hatua nzuri na wananchi wangu kuchangia sehemu ndogo, ni jambo la kushukuru” alishukuru mwenyekiti huyo.

Aidha, Mwenyekiti Maligo alisema pamoja na mchango wa mabati 100, Prof. Muhongo pia alitoa mifuko 50 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hiyo na chumba kimoja cha darasa ambacho pia kimekamilika na kuezekwa kwa mabati 54 kati ya hayo yalitolewa na mbunge.

Hata hivyo mwalimu wa shule ya msingi Bukumi Mabuba Makene alisema, kukamilika kwa nyumba hiyo ni hatua nzuri ya kupunguza tatizo la uhaba wa nyumba za watumishi shuleni hapo.