MWENGE WA UHURU WAWASILI MUSOMA VIJIJINI, MIRADI YAZINDULIWA

Pichani ni mwenge wa uhuru baada ya kuwasili kwenye viwanja vya kijiji cha Chirorwe kwa ajili ya uzinduzi na kuweka jiwe la msingi wa zahanati ya kijiji hicho.

Na. Verdiana Mgoma

MSAFARA wa mbio za mwenge wa Uhuru umewasili kwenye Jimbo la Musoma vijijini na kufanikiwa kukimbizwa kwenye baadhi ya vijiji vya jimbo hilo.

Mbio za mwenge kwa mwaka huu zina kauli mbiu ya “shiriki kukuza uchumi wa viwanda kwa maendeleo ya nchi yetu” ambapo ndani ya jimbo hilo miradi ya maendeleo na huduma za kijamii zimezinduliwa na nyingi zitaendelea kuzinduliwa kwa kipindi ambacho mwenge huo utakuwepo.

Akizungumza katika uzinduzi wa zahanati ya kijiji cha Chirorwe, kiongozi wa mbio za mwenge mwaka huu Amour Hamad Amour amewataka watanzania kuweka nguvu katika kujenga taifa la viwanda ili kutimiza azma ya serikali ya awamu ya tano ambayo imedhamiria kuinua uchumi kwa kujenga viwanda.

Amour alisema, wananchi wanapaswa kujikita katika kilimo ili kuwepo kwa ajira ya kukuza uchumi wa viwanda na kusisitiza kuwajibika na kuepukana na uvivu na kufanya kazi kwa mazoea.

“Kila mmoja wetu anapaswa kuwajibika katika ujenzi wa taifa na kujiepusha na vitendo ambavyo vinaweza kurudisha maendeleo ya taifa nyuma” alisisitiza Amour na kuongeza kuwa, hayo hayatofanikiwa ikiwa watanzania watasumbuliwa na maradhi na kuwataka kuongeza mapambano dhidi ya malaria kwa kutumia vyandarua kujikinga na mbu waenezao ugonjwa huo.

“Pia tujiepushe na rushwa, tujikinge na ugonjwa wa Ukimwi na mapambano dhidi ya madawa ya kulevya hasa kwa vijana ambao hawajatumbukia katika matumizi ya dawa za kulevya, wasijiingize kwenye matumizi ya dawa hizo” alisema Amour Hamad Amour.

Hata hivyo, Kiongozi huyo wa mbio za mwenge alielezea miradi mbalimbali iliyotekelezwa kwa kushirikiana halmashauri pamoja wahisani ambayo itazinduliwa wakati wa mbio hizo.

Moja ya miradi hiyo ni uzinduzi wa kituo cha afya cha Murangi ambao umefadhiliwa na Japan ikiwa ni ishara ya urafiki kati ya Tanzania na nchi hiyo.

Ujenzi wa zahanati hiyo ulihusisha nyumba mbili za wafanyakazi wa kituo hicho, ujenzi wa miundo mbinu ya hospitali ambayo ni choo cha wagonjwa, sehemu ya kuhifadhia takataka na sehemu ya kutupa takataka.