MBUNGE WA MUSOMA VIJIJINI AFANIKISHA NDOTO YA MWANANCHI WA KIRIBA

Johnson Nyeura akiwa nje ya nyumba yake ambayo ujenzi wake umefikia kwenye hatua nzuri.

Na. Ramadhan Juma

BAADA ya kuishi kwenye ofisi ya kijiji cha Kiriba kwa muda mrefu akiwa na familia yake kwa kukosa makazi, mlemavu wa ngozi Johnson Nyeura amehamia kwenye nyumba yake.

Nyeura amefanikiwa kukamilisha nyumba yake kwa msaada wa Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo ambaye alijitolea kumsaidia baada ya kumkuta akiishi kwenye ofisi hiyo ya kijiji.

Kwasasa Nyeura anaishi kwenye nyumba yake ambayo kwa kiwango kikubwa imekamilika na tayari imefungwa hanamu, milango na madirisha na kazi iliyobakia ni kupigwa lipu na sakafu.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi akiwa nyumbani kwake, Nyeura alimshukuru Prof. Muhongo kwa msaada aliompatia na kufanikisha ndoto yake ya kuishi kwenye nyumba yake.

Hata hivyo, Johnson Nyeura licha ya furaha aliyonayo ya kupata makazi hayo, aliomba msaada wa kujengewa choo kwani hivisasa yeye na familia yake wanalazimika kupata huduma hiyo kwa majirani.