NYUMBA ZA WAGANGA ZAZINDULIWA KITUO CHA AFYA MURANGI

Mkuu wa WIlaya ya Musoma vijijini Dkt. Vincent Naano Anney (wa kwanza kulia), Balozi wa Japan nchini Masaharu Yoshida na Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo wakifungua kitambaa kwenye jiwe la msingi kuhashiria uzinduzi rasmi wa nyumba za waganga wa kituo cha afya cha Murangi ambazo zimejengwa kwa ufadhili wa serikali ya Japan kwa gharama ya milioni 170.

Na. Fedson Masawa

NYUMBA kwa ajili ya makazi ya waganga wa kituo cha afya cha Murangi zimezinduliwa rasmi leo kijijini hapo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na kijiji hicho.

Uzinduzi huo ulioongozwa na Mbunge wa Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo, ulihudhuriwa pia na Balozi wa Japan nchini Masaharu Yoshida, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma vijijini Charles Magoma, Mkuu wa Wilaya ya Musoma Dkt. Vincent Naano Anney, madiwani na viongozi mbalimbali wa kijiji hicho.

Akizungumza baada ya uzinduzi huo, Prof. Sospeter Muhongo aliwashukuru serikali ya Japan kwa kufadhili mradi huo mkubwa wenye lengo la kuboresha huduma za afya kituoni hapo uliogharimu milioni 170 huku akitumia hadhara hiyo kusisitiza kuendelea kwa kasi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Wananchi mbalimbali waliozungumza na mwandishi wa habari hizi, walishukuru wote waliofanikisha ujenzi huo ambao walisema utawasaidia kupata huduma ya uhakika na haraka wakati wowote tofauti na awali ambapo walipata wakati mgumu kutokana na waganga kuishi mbali na eneo hilo na hivyo kukosa huduma ya haraka inapotokea dharura.

Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo akihutubia wananchi wake (hawapo pichani) waliohudhuria kwenye sherehe za uzinduzi wa nyumba za waganga wa kituo cha afya cha Murangi huku viongozi wengine wakimsikiliza kwa makini.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma vijijini Charles Magoma akimkabidhi zawadi Balozi wa Japan nchini Masaharu Yoshida wakati wa sherehe za uzinduzi wa nyumba za waganga wa kituo cha afya cha Murangi huku zoezi hilo likishushudiwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mbunge wa Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo.

Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Murangi waliohudhuria sherehe za uzinduzi wa nyumba za waganga wa kituo cha afya wakishangilia na wengine wakifuatilia kwa makini hotuba za viongozi mbalimbali waliopata nafasi ya kuzungumza kwenye sherehe hizo ambazo zilifana.