RUSOLI WAKARIBISHA OFISI YA MBUNGE KUKAGUA MASHAMBA YAO

Mbunge wa viti maalum Agness Chinuno (aliyesimama) akizungumza na baadhi ya wakulima wa bustani baada ya kuvuna nyanya tayari kwenda sokoni.

Na. Mwandishi Wetu

VIKUNDI vya vijana na akina mama Musoma vijijini vimekaribisha uongozi wa ofisi ya mbunge kufika katika mashamba yao yaliyoko katika kata ya Rusoli kwa ajili ya kujiridhisha na hatua iliyofikiwa na vikundi hivyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu, Diwani wa kata ya Rusoli Boazi Nyeula alisema, kata ya Rusoli peke yake ina mashamba makubwa ya kutosha huku kukiwa na vikundi vingi vinavyojishughulisha na kilimo cha bustani za mbogamboga na matunda, lakini wanashindwa kupanua mashamba hayo kutokana na upungufu wa vitendea kazi.

Boazi alisema, pamoja na changamoto hizo, kati ya vikundi hivyo vinavyojishughulisha na kilimo hicho ni kikundi kimoja peke yake kwenye kata yake kilichojitahidi kwa sasa kununua mashine ya kumwagilia na mipira, vikundi vingine vilivyobakia vinatumia ndoo kumwagilia bustani zao.

Diwani wa viti maalum Agness Chinuno aliyeongozana na Msaidizi wa Mbunge katika mashamba hayo ya bustani, alisema kata ya Rusoli ni moja ya kata zilizo na mashamba ya kutosha kulima bustani na hilo linadhihirika kutokana na hali halisi iliyopo, ambapo vipo vikundi vitatu vimeanza kuandaa mashamba yenye ukubwa wa hekari sita kwa ajili ya kilimo cha matikiti maji, lakini bado yapo mashamba mengine ya kutosha.

Mbunge huyo alisema, mwanzoni wananchi wa kata hiyo hawakuwa na hamasa yoyote kuhusu kilimo cha bustani, lakini kwa sasa akina mama wengi na vijana wamekimbilia kwenye vikundi na ndio maana wamefikia hatua baadhi waliotangulia kununua mashine ya kumwagilia.

Mmoja wa vijana wanaojishughulisha na kilimo cha bustani Malofu Mjinja alisema, vijana wanawaza kupanua zaidi maeneo ya kilimo chao na tayari kazi imeanza katika mashamba yaliyo kandokando mwa ziwa, lakini changamoto kubwa inayowakabili ni ukosefu wa zana za kuwarahisishia kazi ikiwemo mashine za kumwagilia, na kuahidi iwapo watapata watahakikisha hakuna njaa katika kata ya Rusoli na maeneo ya jirani.

“Tunakushukuru sana ndugu yetu maana umesikia wito wetu na kama tumekuona wewe basi tunajua tumefikiwa na Prof. Sospeter Muhongo ambaye ni Mbunge wetu. Kilio chetu kikubwa kwako ni kwamba tuna malengo ya kujilisha wenyewe Musoma Vijijini kwa maana maeneo makubwa tunayo, nguvu tunazo na tunaomba Mbunge na serikali watusaidie vitendea kazi na mashine ili kurahisisha kazi” alishukuru na kuomba Mjinja.

Hata hivyo, Masami Lucas ambaye ni moja kati ya wanavikundi wa kata ya Rusoli alisema, kikundi chao kwa sasa kipo katika mavuno ya nyanya na wanamshukuru mwenyezi Mungu kwani mavuno yao yametoka vizuri na sasa wanaelekea kuanza msimu mwingine.

Masami aliomba Mbunge wao kuwawezesha katika vitendea kazi na mbegu bora kama alivyofanya katika vikundi 15 vya jimbo la Musoma vijijini ili waweke nguvu hizo pamoja wataweza kulilisha jimbo.

“Prof. Muhongo ni Mbunge wa watu, tunaamini kama akijitahidi kutuwezesha kama alivyofanya kwa vikundi 15, basi tukiunganisha nguvu zetu kama wanavikundi jimbo zima na maeneo tuliyo nayo yenye maji ya kutosha, Musoma vijijini hatutazungumzia ukosefu wa chakula” alisema Lucas.

Kwa upande wake Msaidizi wa Mbunge Fedson Masawa, aliwapa pole na kuwapongeza vijana na akina mama hao kwa mipango yao na malengo yao mazuri waliyo nayo na kuwahasa waendelee na jitihada hizo huku wakisubiri taratibu nyingine za vifaa zikifanyika.

“Ndugu zangu wana Rusoli, poleni na hongereni sana kwa mipango na malengo mazuri ama kweli mmeona mbali, kweli tukiamua tutajilisha wana Musoma vijijini. Jimbo letu lina vikundi vingi na kusema ukweli si rahisi Mbunge kutusaidia kwa wakati mmoja na mkilinganisha na miradi anayoendelea kuitekeleza kwenye sekta ya elimu hasa ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi Jimboni” alisema Masawa.

Msaidizi huyo wa mbunge aliongeza: “Kutokana na wingi wa vikundi vilivyopo Jimboni, kitakachowezekana basi Mbunge atakifanyia kazi na taarifa ya maombi yenu nitaifikisha. Lakini pia ikitokea mmesaidiwa vifaa hivyo, basi nanyi mjitume zaidi kuhakikisha vifaa vinavyotolewa na Mbunge vina uwezo wa kufanyiwa kazi na kunufaisha walioko ndani na nje ya vikundi hasa matokeo ya mwisho wa shughuli zenu.”