ZOEZI LA UPIMAJI WA ENEO LA ZAHANATI BURUNGU LAKAMILIKA

Viongozi wa serikali ya kijiji, kata na Halmashauri wakijadiliana mara baada ya kukamilika kwa zoezi la upimaji wa eneo ambalo itajengwa zahanati ya kitongoji cha Burungu.

 Na. Fedson Masawa

MGANGA Mkuu wa Wilaya ya Musoma Dkt. Thadeus Makwanda amehudhuria zoezi maalum la upimaji wa eneo linalotarajiwa kujengwa zahanati katika kitongoji cha Burungu, kijiji cha Bukumi kata ya Bukumi.

Zoezi hilo liliongozwa na Mhandisi wa wilaya aliyekuwa ameambatana na Mganga Mkuu wa wilaya ya Musoma pamoja na viongozi mbalimbali kutoka Halmashauri ya wilaya ya Musoma akiwemo Afisa ardhi kutoka Halmashauri ya Musoma.

Akizungumzia hali halisi ya eneo lililopimwa kwa ajili ya zahanati, mhandisi Mkuu wa wilaya Maige Gibai alisema, eneo lililotengwa na kijiji ni kubwa na linatosheleza kujenga zahanati pamoja na nyumba za waganga.

Maige aliwaomba wananchi wajitume na kuanza kusogeza mawe, matofali, kototo na mchanga wakati wakisubiri mchoro ili kuhakikisha zoezi la ujenzi linaenda kwa kasi na serikali ianze kuiweka zahanati yao kwenye bajeti.

Naye Mganga Mkuu Dkt. Thadeus Makwanda alisema, wananchi wameteseka kupata huduma hiyo kwa kutembea umbali mrefu kuifuata jambo ambalo hapendi kuliona likiendelea, kwani hali hiyo ndio inayochangia vifo vingi vya akinamama wajawazito, watoto na wazee.

“Ndugu wananchi mmeteseka sana, namimi sipendi muendelee kuteseka. Unakuta mama anaumwa na uchungu usiku, akikaa kuanzia saa 3 hadi saa 4 bila huduma yoyote na hasa ikitokea kama mimba ina matatizo, basi tunaweza kumpoteza mtoto au mama” alisema Dkt. Makwanda.

Aidha Dkt. Mwakwanda aliongeza kuwa, kwa sasa wananchi wanatakiwa waungane ili kuhakikisha zoezi la ujenzi linaenda kwa kasi na wawe na hali ya kuhamasishana kutoa michango mbalimbali pamoja na kushiriki katika zoezi zima la ujenzi.

“Kwahiyo sasa mnatakiwa muwe na moyo kweli kweli. Muwe na Moyo wa kuhamasishana, kuchanga na kujenga. Vyote hivyo mkiwa navyo hii zahanati haichukui miaka mingi” alisema Dkt. Makwanda.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa kijiji cha Bukumi na kitongoji cha Burungu, Magreth Deus ambaye ni mkazi wa eneo hilo,  alishukuru ujio wa serikali kwa lengo la kuwasogezea huduma karibu.

Magreth alisema, huduma hiyo ilikuwa ikisubiriwa na kuhojiwa kwa kipindi kirefu kupitia kwa viongozi wao, hivyo jukumu lao sasa ni kutekeleza maagizo ya wataalamu, kusogeza mawe, mchanga na michango mingine inayohitajika na kuwaomba wataalamu wawaishe ramani ya majengo hayo ili ujenzi uanze mapema.

“Kwa niaba ya wananchi wa eneo hili, ninapenda kuwashukuru sana wataalamu kwa kuja kusogeza huduma hii. Pia jukumu letu sasa ni kutekeleza maagizo mliyotuagiza. Tutasomba mchanga, matofali na tutachanga kwa kuhamasishana” alisema Magreth.

Akifunga kikao hicho cha wataalamu na wananchi kilichofanyika baada ya zoezi la upimaji wa eneo la zahanati, Mwenyekiti wa kijiji cha Bukumi Nyaonge Maligo alishukuru idara ya afya, ardhi na ujenzi kwa kuona umuhimu wa kufika na kuthibitishia wananchi wake kwa vitendo kwamba, sasa kazi ya ujenzi wa zahanati imeanza.