MATARAJIO YA KUPATA MBEGU BORA YA MIHOGO YAANZA KUONEKANA MUSOMA VIJIJINI

Moja ya mashamba ya mbegu za mihogo yaliyostawi vizuri katika kijiji cha Maneke.

Na. Ramadhani Juma

MSAADA wa mbegu za mihogo zilizotolewa na Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa ajili ya kuzalisha  mbegu za ziada katika mashamba darasa, zimeanza kuonesha mafanikio katika baadhi ya maeneo ndani ya jimbo hilo.

Katika maeneo mbalimbali ikiwemo kijiji cha Maneke, mbegu hizo zimestawi vizuri na kuleta matumaini ya kuwapo kwa mbegu za kutosha kwa siku za usoni.

Kaimu Afisa Kilimo Wilaya ya Musoma vijijini, Godfrey Nyambwe akizungumza baada ya kukagua mashamba ya mbegu, alimshukuru Afisa Kilimo wa kijiji hicho Mwaliki Muyengi kwa jinsi alivyosimamia kazi zake vizuri hadi wananchi wa kijiji hicho kuvunja rekodi ya kustawisha mbegu bora za mihogo.

“Nakushukuru sana ndugu Muyengi kwa jinsi ulivyosimamia mbegu hizi tangu mwanzo wa ugawaji, upandaji na sasa zimestawi vizuri, pia niwashukuru wana kikundi wa Keuma na Mzee Mafuru Geremo walivyoamua kutengeneza mashamba darasa kwa ajili ya kustawisha mbegu hizi, hivyo nawaomba wazitunze mbegu hizo hadi pale zitakapotosha kuvunwa” alisema Nyambwe.

Katika kijiji hicho cha Maneke, Jumla ya heka tatu za mihogo zimestawishwa katika mashamba darasa mawili, ambapo heka moja na nusu imestawishwa na mkulima binafsi Mafuru Geremo na heka nyingine moja na nusu imestawishwa na kikundi cha Keuma.