VIKUNDI VYA BURUDANI VYANOGESHA ZIARA YA MAKAMU WA RAIS

Kikundi cha Kwaya kutoka Kata ya Bugoji wakitumbuiza katika uwanja wa Mukendo, Manispaa ya Musoma wakati wa ziara ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani.

Na. Ramadhan Juma

VIKUNDI vya burudani kutoka jimbo la  Musoma vijijini, vimekonga nyoyo za wengi katika ziara ya Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassani wilayani Musoma.

Vikundi hivyo vilipata nafasi ya kutumbuiza katika maeneo mbalimbali, ambapo kikundi cha ngoma kilipata nafasi ya kutumbuiza wakati wa uzinduzi wa barabara ya lami Kilomita 9.9 kutoka Buhare hadi Mutex na kilipata nafasi tena katika uwanja wa Mukendo wakati wa mkutano wa hadhara.

Kikundi cha kwaya kilipata nafasi ya kutumbuiza kabla ya mkutano na baada ya mkutano huo uliofanyika katika uwanja wa Mukendo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, washiriki wa vikundi hivyo, kikundi cha ngoma (Kiwajaki) kutoka kata ya Kiriba na kikundi cha kwaya kutoka kata ya Bugoji, wamemshukuru Mbunge wao Prof. Muhongo kwa kuwapatia fursa ya kuonyesha vipaji vyao.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa mbunge kwa kutupa nafasi ya kuja kuonyesha vipaji vyetu, hakika tunaweza, tunamwomba aendelee kutufadhili hata kwenye matamasha ya kitaifa tuwaonyeshe watanzania uwezo wa Musoma vijijini, hatutamwangusha milele. Tunajiamini” alisema Wanyanja Masatu, kiongozi wa kikundi cha ngoma.