VIKUNDI VYA NGOMA NA KWAYA KUPAMBA ZIARA YA MAKAMU WA RAIS MUSOMA

Kikundi cha ngoma cha Bwai kinachotarajiwa kutumbuiza kwenye mapokezi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani anayetarajia kuwasili Wilayani Musoma 7, Juni mwaka huu.

Na. Mwandishi Wetu

VIKUNDI vya ngoma na kwaya kutoka kijiji cha Bugoji na Bwai vinatarajia kupamba mapokezi ya Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassani anayetarajia kuwasili wilayani Musoma 7, Juni mwaka huu.

Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo ameahidi kuchangia usafiri na chakula kwa vikundi hivyo ili vikatoe burudani kwenye mapokezi hayo.

“Kwaya ya Jimbo (kutoka Kijiji cha Bugoji) na Kikundi cha Ngoma (kutoka Kijiji cha Bwai) cha Jimbo la Musoma Vijijini vitatumbuiza siku hiyo ya Ugeni huo mkubwa Wilayani mwetu.  Tudumishe Utamaduni wetu na Tujitume” alisema Prof. Muhongo.

Vikundi hivyo maalum viwili vilipatikana kwenye michuano ya ngoma na kwaya ya kilele cha sherehe za nane nane za mwaka jana zilizofanyika kwenye kijiji cha Suguti.