SHEHENA NYINGINE YA VITABU YAWASILI MUSOMA VIJIJINI

Na. Mwandishi Wetu 

KONTENA la futi 40, lenye vitabu zaidi ya 22,000 limewasili Musoma vijijini kwa ajili ya kusambazwa kwenye shule za sekondari za jimbo hilo.

Vitabu hivyo vyenye thamani ya dola za Kimarekani 350,000 vitatolewa bure kwenye shule za Sekondari (20) na Msingi (111).

Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo, amewahimiza wakuu wa shule mbalimbali za jimbo hilo na viongozi wa serikali zilipo shule hizo kukamilisha ujenzi wa maktaba na wale ambao hawajaanza, waanze ujenzi ili wapate mgao wa vitabu hivyo.

Prof. Sospeter Muhongo alisema, muda bado upo kwa ajili ya zoezi hilo kwani vitabu hivyo vitaanza kugawiwa 1, Januari 2018 na moja ya vigezo vya kupata mgao ni kuwa maktaba ya kuhifadhi vitabu hivyo.

Hii ni mara ya 5 kwa shule za jimbo hilo kupokea vitabu kutoka Marekani na Uingereza ambapo vitabu vingi ni kwa ajili ya masomo ya Sayansi na Kiingereza, lengo likiwa ni kuwaongezea wanafunzi uelewa na kupandisha kiwango cha ufaulu ndani ya jimbo hilo.

Shule mbalimbali tayari zimepokea vitabu hivyo kwa awamu zilizopita, ambapo mbali na shule za Jimbo la Musoma vijijini, shule nyingine za Mkoa wa Mara zimefaidika na mgao huo.

Mwaka jana, Prof. Muhongo alikabidhi vitabu vya sayansi na hesabu 25,000 vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 500 kwa wabunge wote wa Mkoa wa Mara kwa ajili ya shule za msingi na sekondari mkoani humo.

Wabunge waliokuwepo kwenye makabidhiano hayo ni Ester Matiko (Tarime Mjini, Chadema), John Heche (Tarime Vijijini, Chadema), Boniphace Mwita (Bunda Vijijini, CCM), Kangi Lugora (Mwibara, CCM) na ambao hawakufika walituma wawakilishi.