MUSOMA VIJIJINI WAHAMASISHWA KULIMA ZAO LA DENGU

Baadhi ya wanachama wa kikundi cha Suguti farmer’s wakiwa katika zoezi la umwagiliaji wa dawa katika shamba la dengu. Katikati (mwenye fulana nyeusi) ni Afisa kilimo wa kijiji cha Kusenyi, Majura Chikumbiro akitoa maelekezo ya kitaalamu kwa wakulima hao.

 Na. Verediana Mgoma

KIKUNDI cha Suguti Farmer’s kilichopo kwenye kijiji cha Kusenyi wamejitosa kulima zao la dengu ili kuhamasisha wanakijiji wenzao kulima zao hilo.

Kiongozi wa kikundi hicho Mathayo Masatu alisema, wameamua kulima zao hilo kutokana na kuwepo tabia ya jamii yetu kuzoea kulima msimu, badala yake wao wanalima msimu wote hata kukiwa hakuna mvua.

Masatu alisema, shamba lao wanatarajia litakuwa darasa ambalo linaweza kuwavutia walio wengi na kujikita zaidi kwenye kilimo bila ya kujali msimu.

“Sisi vijana tumeona ni vyema tukawa waanzilishi kwenye suala zima la kilimo na mpaka sasa tumelima heka tatu za alizeti tulizopokea kutoka ofisi ya mbunge, pia tumelima heka moja ya maharage na hizo heka nne za dengu ambazo tuna imani haya ni baadhi ya mashamba darasa tulioamua kuanza nayo” alisema kiongozi huyo na kuongeza kuwa, wapo tayari kuelimisha na kuhamasisha watu kujikita zaidi kwenye kilimo bila kusubiri.

Afisa kilimo kijiji cha Kusenyi, Majura Chikumbiro akizungumzia zao hilo la dengu alisema ni moja ya nafaka kama zilivyo nafaka nyingine na ni miongoni mwa zao muhimu kwa biashara pia hulimwa ukanda wa ziwa.

Chikumbiro alisema, dengu hutumika kama mboga mchanganyo wa wali mseto na makande na kwa upande wa kanda ya ziwa hili ndio zao linalotegemewa zaidi likiongozwa na choroko kwa kuwa na thamani kubwa hivyo zao hilo ni muhimu kwa uchumi wa kanda ya ziwa.

“Kilimo hiki hakina usumbufu kama yalivyo mazao mengine hasa ukifuata taratibu, hupendelewa kulimwa zaidi kwenye maeneo ya mbuga ambayo huwahi kukauka, hivyo msimu mzuri wa kilimo cha dengu ni mwezi wanne mwishoni au wa tano mwanzoni kuhusu soko la dengu ni uhakika zaidi kwa maana uhitaji wake ni nje na ndani ya nchi” alisema Majura Chikumbiro.