VIJANA WA MUSOMA VIJIJINI WAAHIDI KUJIAJIRI BAADA YA MAFUNZO

Vijana wa jimbo la Musoma vijijini wakiendelea na mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua, pichani wanaonekana wakiwa katika hatua ya uunganishaji wa mfumo wa betri, taa na seli za sola katika kituo cha Murangi.

Vijana wa jimbo la Musoma vijijini wakiendelea na mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua, pichani wanaonekana wakiwa katika hatua ya uunganishaji wa mfumo wa betri, taa na seli za sola katika kituo cha Murangi.

Na Fedson Masawa

VIJANA wanaopata mafunzo ya utengenezaji wa taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua katika kituo cha Murangi, wameahidi kujiajiri baada ya kumaliza mafunzo yao.

Wakingumza na mwandishi wa habari hizi, vijana hao wamempongeza mkufunzi wa mafunzo hayo Dkt. Hong-kyu Choi kutokana na jinsi anavyowafundisha na kuelewa.

Awali, akizungumza na wasimamizi wa mafunzo hayo, Ester Charles kijana kutoka kijiji cha Ryasembe kata ya Murangi, alisema anatarajia kutoka na ujuzi ambao utamsaidia kujiajiri na si kutegemea kuajiriwa tena.

“Ninafurahi sana kushiriki mafunzo haya, na kwa namna tunavyoendelea naamini binafsi ninatarajia kutoka hapa na ujuzi utakaoniwezesha kutengeneza ajira binafsi, siyo kutegemea kuajiriwa na mtu” alisema Ester.

Naye, Mugenyanda Mbasa kijana kutoka kata ya Rusoli, alimshukuru Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa kuwaona vijana wake jimboni na kuwatengenezea fursa zinazowapelekea kujiajiri na hivyo ujuzi watakaoupata katika mafunzo hayo utakuwa ni taa bora itakayowasaidia kumulika maisha yao yajayo.

“Binafsi nimshukuru sana mbunge wetu wa jimbo la Musoma vijijini kwa namna alivyotupa fursa tunayoweza kutumia na kuleta mabadiliko jimboni. Pia mafunzo aliyoyaanzisha ni taa itakayotusaidia kumulika maisha yetu ya usoni” alishukuru Mbasa.

Kijana mwingine Elisha Morice, kwa upande wake aliwahimiza vijana wenzake wanaoendelea na mafunzo, waliokwisha kamilisha na wale ambao hawajaanza mafunzo kuwa mwisho wa mafunzo hayo uwe ni mwanzo wa kueneza na kusambaza ujuzi huo kwa vijana wenzao ambao hawakupata fursa ya kushiriki mafunzo hayo ili kupunguza utegemezi na uzururaji kwa vijana wa Musoma vijijini.

“Ndugu zangu, mimi napenda pia kuwahimiza vijana wote tunaoendelea na mafunzo, waliokwisha hitimu na wale ambao hawajaanza kwamba, mwisho wa mafunzo haya uwe ni mwanzo wa mafunzo kwa vijana wenzetu ambao hawakubahatika kushiriki mafunzo haya ili kuondokana na utegemezi na uzururaji” alisema kijana Elisha, anayetoka kijiji cha Chumwi.

Naye, Mkufunzi wa mafunzo hayo Dkt. Hong-kyu Choi kutoka Korea, amewasihi vijana kuwa wepesi wa kubadili mtazamo wao, fikra na kujiamini kwa kujali kile anachowafundisha kwani Prof. Muhongo ambaye ni mtu pekee aliyewafanya wafike jimboni hapo na Tanzania kwa ujumla ana nia njema na jamii yake na anaweza kuwasaidia na kuwainua vijana endapo wakiwa tayari kubadilika ili kuondokana na umaskini kwa kujitengenezea ajira binafsi.