VIJANA 100 KUPATA MAFUNZO YA KUTENGENEZA VIFAA VYA UMEME JUA

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa pili kulia) akionesha vifaa vya umeme jua ambavyo Balozi wa Korea nchini anatarajiwa kupeleka mtaalamu jimboni humo ili kuwafundisha vijana namna ya utengenezwaji wake.

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa pili kulia) akionesha vifaa vya umeme jua ambavyo Balozi wa Korea nchini anatarajiwa kupeleka mtaalamu jimboni humo ili kuwafundisha vijana namna ya utengenezwaji wake.

Na. Mwandishi Wetu

UBALOZI wa Korea Kusini nchini, unatarajia kutimiza ahadi yake iliyotolewa na balozi Song, Geum-Young kuwapatia mafunzo yatakayozalisha ajira vijana wa Musoma vijijini waliohitimu Kidato cha Nne.

Balozi Song, Geum-Young alitoa ahadi hiyo mwishoni mwa mwaka jana, ambapo aliahidi kumpeleka jimboni humo mtaalamu kwa ajili ya kuwafundisha vijana namna ya kutengeneza taa na chaja ndogo kwa ajili ya kuchaji simu zinazotumia mionzi ya jua.

Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini, Prof. Sospeter Muhongo kupitia taarifa yake, alisema Dk. Hong K Choi kwa kushirikiana na Ubalozi wa Korea Kusini watatoa mafunzo hayo kwa vijana 100 kutoka jimboni mwake.

Prof. Muhongo alisema, vijana watakaopata nafasi hiyo ni wale waliomaliza kidato cha nne na wanaoishi kwenye vijiji vya jimbo hilo.

“Mafunzo yaanza tarehe 20 Feb 2017, Kijijini Nyegina. Wasaidizi wa Mbunge na Madiwani watachagua vijana watakaohudhuria mafunzo hayo” alisema Prof. Muhongo na kuongeza kuwa, kifaa hicho kikitengenezwa gharama yake ni 15,000, hivyo vijana watapewa mafunzo ya namna ya kuvitengeneza na watauza ili kujipatia kipato.