WANANCHI KIJIJI CHA KIEMBA WAENDELEA KUJENGA MAKAZI MAPYA

 

Kiemba 1

 

Na. Juma Shabani

WANANCHI wa kijiji cha Kiemba kata ya Ifulifu, wanaendelea na ujenzi wa nyumba mpya baada ya zile za awali kubomolewa na upepo mkali uliokikumba kijiji hicho miezi michache iliyopita.

Wananchi hao walianza ujenzi huo baada ya kupokea vifaa mbalimbali kutoka kwa mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ambaye aliahidi kutoa msaada huo alipotembelea kijijini hapo mwishoni mwaka jana.

Wakizungumza kijijini hapo, wananchi hao walimshukuru mbunge wao kwa kuwasaidia na kuwaondoa kwenye mazingira magumu waliyokuwa nayo baada ya nyumba zao kubomoka na nyingine kuezuliwa mabati na upepo mkali uliombatana na mvua kubwa.

“Nilikuwa na hali mbaya baada ya nyumba yangu kubomoka yote na kuishia chini na vyombo vyangu vya ndani kuharibika kabisa, nikakosa mahala pa kujihifadhi, nikawa naomba kwa majirani leo hapa kesho pale, lakini baada ya mbunge wetu kupata taarifa hizo kupitia kwa wasaidizi wake, aliweza kufika sehemu ya tukio na kujionea kilichotokea na kutuhaidi vifaa vya ujenzi siku hiyo hiyo nilipokea vifaa vya ujenzi ikiwa ni mabati, saruji na misumari” alisema Nyakaita Magati.

Magati aliendelea kusema: “hivi sasa nyumba imefikia kwenye hatua ya renta, naelekea kukamilisha nyumba yangu, kwa kweli tunamuomba mbunge wetu aendelee na moyo huo huo na Mungu ambariki sana pamoja na wasaidizi wake”

Naye, Tatu Richard alithibitisha kupokea vifaa vya ujenzi kutoka kwa mbunge na sasa nyumba yake imekamilika, jambo ambalo awali hakuamini kama lingewezekana.

“Jamani mimi mjane sijui ningefanyaje, niliona maisha yangu sasa yamekuwa magumu kupitiliza baada ya nyumba yangu kuezuliwa paa lote na kutupwa pembeni, sikuwa na mtu wa kunipa msaada kabisa, lakini Mungu sio Athumani, nilishangaa baada ya kuona watu wengi sana wakija kwangu na nikamuona mbunge wetu akiwa amefika kwangu kunipa pole na kunikabidhi vifaa vya ujenzi” alisema Tatu.

Mwandishi wa habari hizi alizungumza na wananchi wengine ambao aliwakuta kwenye maeneo yao wakiendelea na ujenzi wa makazi yao mapya na kurekebisha nyumba zilizopata nyufa, ambapo wamesema zoezi hilo litakamilika ndani ya mwezi mmoja na nusu.