SHULE YA MSINGI KURUKEREGE WAPOKEA MIFUKO 180 YA SARUJI

Untitled

Diwani wa Nyegina Majira Mchele (kushoto) akiwa na mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kurukerege Justine Masige, baada ya kupokea mifuko 180 ya saruji  kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Na Juma Shabani

WANANCHI wa kijiji cha Kurukerege wamepata matumaini ya kukabiliana na tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa, baada ya kupokea mifuko 180 ya saruji kutoka kwa mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo.

Mmoja wananchi wa kijiji hicho Justine Bugingo, akizungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini hapo, alimshukuru mbunge huyo kwa kuona changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa na kuitafutia ufumbuzi.

“Tumekuwa na changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa katika shule yetu, ila sasa kwa juhudi za mbunge wetu ametufanya kuwa miongoni mwa watu ambao sasa tunaona mwanga mkubwa wa maendeleo jimboni kwetu” alisema Bugingo.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kurukerege Justine Masige alisema: “mimi na walimu wenzangu wote tutahakikisha tunasimamia suala la ujenzi wa vyumba vya madarasa, watoto wetu wameteseka kwa muda mrefu sana kwa kusomea nje na kusababisha kiwango cha elimu kushuka kutokana na mazingira na hali ya hewa mfano jua, mvua na upepo”

Kwa upande wake diwani wa kata ya Nyegina, Majira Mchele alithibitisha kupokea mifuko 180 ya saruji ndani ya kata yake na kumshukuru Prof. Muhongo kwa hatua hiyo inayoonyesha wazi nia yake ya kutatua tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari ndani ya jimbo hilo.

“Shukrani nyingi sana zimfikie mheshimiwa mbunge, hii ni heshima kubwa sana anayotufanyia ndani ya kata, ninachoweza kusema ni kwamba, hakuna kitakacho haribika, nitahakikisha na nitasimamia vyema kabisa ujenzi wa vyumba vya madarasa yaliyo bora kabisa” alisema diwani huyo na kuongeza kuwa, atahakikisha saruji hiyo inafanya kazi iliyokusudiwa haraka.