MIFUKO 2,560 YA SARUJI YAWASILI MUSOMA VIJIJINI, YAANZA KUSAMBAZWA

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Chumwi Lucia Mjengwa (kushoto) akiwa na wanafunzi wake Mfungo Manyama (katikati) na Mafwiri Yohana muda mfupi baada ya kupokea saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa shuleni kwao.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Chumwi Lucia Mjengwa (kushoto) akiwa na wanafunzi wake Mfungo Manyama (katikati) na Mafwiri Yohana muda mfupi baada ya kupokea saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa shuleni kwao.

Na Fedson Masawa

MIFUKO 2,560 ya saruji iliyotolewa na Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo imewasili jimboni humo na kupokelewa na wasaidizi wa mbunge.

Saruji hiyo ilianza kuwasili kuanzia 13, January, 2017  imeanza kusambazwa kwenye shule mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule mbalimbali za msingi na sekondari Musoma vijijini ikiwa ni mkakati maalumu wa mbunge wa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa jimboni mwake.

Wakati huo huo Verediana Mgoma anaripoti kuwa, shule ya msingi Chumwi imepokea mifuko ya saruji 120 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa vya shule hiyo yenye upungufu wa vyumba 13.

Mwalimu mkuu wa shule ya Chumwi, Lucia Mjengwa mara baada ya kupokea mifuko hiyo, alimshukuru mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa kutatua changamoto mbalimbali katika sekta ya elimu.

“Tunamshukuru sana mbunge, mpaka sasa tatizo la madawati limekwisha, lakini tuna changamoto kubwa ya upungufu wa vyumba vya madarasa, mpaka sasa shule imegawanywa kutokana na wingi wa wanafunzi, hivyo mahitaji ya vyumba ni 23 vilivyopo ni 10 na upungufu ni 13, kwahiyo tutaitumia saruji hii vizuri na kuanza ujenzi” alisema mwalimu Lucia.

Kwa upande wake mwanafunzi Mafwiri Yohana, alimshukuru mbunge kwa msaada huo ambao utawasaidia kutatua changamoto za vyumba vya madarasa.

“Sasahivi kutokana na uhaba wa madarasa, wakati mwingine tunalazimika kusomea nje na muda mwingine hali ya hewa inapobadilika, inatulazimu kubadilishana muda wa masomo, hivyo endapo changamoto ya vyumba ikipungua tutakuwa huru darasani na kusoma tufike mbali zaidi” alisema mwanafunzi huyo.

Mwenyekiti wa kijiji cha chumwi Mafwele Mkama, akizungumza na mwandishi wa habari hizi alisema, wamejipanga kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa ushirikiano uliopo kati uongozi na wananchi.

“Mimi kama mdhamini mkuu katika kijiji hiki, nitakuwa bega kwa bega na wananchi wangu kumuunga mkono mbunge na kuhakikisha tunafanya vizuri zaidi katika suala la taaluma” alisema mwenyekiti Mkama.

Hadi sasa, miongoni mwa shule zilizopo kata ya Nyamrandirira zilizopokea msaada wa saruji awamu ya kwanza ni pamoja na Rwanga, Nyamrandirira, Chumwi A na B ikiwa jumla ya mifuko ya saruji 240.