KIKUNDI CHA MWANGA WAVUNA MAZAO YAO, WAJIANDAA KUINGIA SOKONI

Untitled

Baadhi ya wakulima wa bustani ya Mwanga (wenye ndoo) wakionyesha mavuno yao kwa viongozi wa TANESCO na Msaidizi wa Mbunge (Mugango) walipotembelea wakulima hao wakati wakiendelea na ziara ya kuchukua takwimu za mahitaji ya umeme kwenye kata ya Nyambono.

 

 

Na. Hamisa Gamba

KIKUNDI cha vijana wanaojishughulisha na kilimo cha bustani kwenye kijiji cha Saragana, wamekamilisha msimu wa kilimo kwa kuvuna nyanya na vitunguu walivyopanda.

Kikundi hicho cha Mwanga (Mwanga Farmers), ni moja ya vikundi vilivyopata mbegu bora na mashine za kumwagilia kutoka kwa mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo.

Mwenyekiti wa kikundi hicho Amos Bwire akizungumza kwa niaba ya wenzake alisema, licha ya mafanikio ya mavuno hayo bado wana changamoto ya ukosefu wa madawa ya kukidhi mahitaji ya mazao.

“Kuna changamoto mbalimbali zinatukabili licha ya mavuno tuliyopata, kubwa ni ukosefu wa madawa kwa ajili ya kuulia wadudu, lakini pia kushuka kwa bei ya nyanya na hali ya hewa kumetuathiri kwenye msimu huu” alisema mwenyekiti Bwire.

Naye mjumbe wa kikundi hicho Magesa Mauna alisema, licha ya changamoto walizokutana nazo kwenye kilimo hicho, bado wataendelea kulima bila kuchoka ili kuunga mkono jitihada za mbunge wa jimbo hilo aliyewahamasisha kuingia kwenye kilimo cha bustani kwa njia ya umwagiliaji.

“Tunaamini mbunge ana nia njema na sisi wakulima wa bustani, hivyo tunaomba pale tutakapokuwa tumekwama katika shughuli zetu za kilimo, aendelee kutuunga mkono kama kauli mbiu yake isemavyo hakuna kushindwa, hakuna kukata tamaa kwani kilimo ni uchumi”  alisema Magesa Mauna huku akinukuu kauli ya Prof. Muhongo.