WAFUGAJI WA MUSOMA VIJIJINI WAENDELEA KUUNDA VIKUNDI VYA UCHUMI: KATA ZA IFULIFU NA NYAKATENDE ZAOMBA JOSHO LAO LA MWAKA 1956 LIBORESHWE

Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo alikaribishwa kutembelea josho na rambo la wafugaji wa Kata za Ifulifu na Nyakatende.

Josho wanalolitumia lilijengwa Mwaka 1956, na kwa sasa linahudumia ng'ombe zaidi ya elfu tano (5) kutoka vijiji saba vya Kata hizo mbili.

Wafugaji wa Kata hizo mbili wameanzisha vikundi kadhaa vya wafugaji, wauzaji maziwa na wakulima wa nyasi za malisho.

Maombi makuu ya wafugaji hao:
(i) Josho la Mwaka 1956 lililojengwa Kijijini Kabegi liboreshwe kwa kuziba nyufa, na liwe la kisasa

(ii) Chanzo cha maji: rambo la Kijijini Kabegi limejaa tope na kingo za kuta zimebomoka hazipo

Mbunge wa Jimbo ameahidi kufikisha maombi hayo Serikalini.

Vilevile, Mbunge huyo aliwagawia wanavijiji vitabu viwili viwili vinavyoelezea mafanikio makubwa yanayopatikana Jimboni mwetu kutokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2020-2025

Vyanzo vya mapato ya wananchi wa Jimboni mwetu ni:
(i) Kilimo cha pamba, na cha mazao ya chakula (mihogo, mahindi, mpunga, viazi vitamu, alizeti, mbogamboga na matunda)

(ii) Uvuvi wa samaki ndani ya Ziwa Victoria na kwenye baadhi ya mito

(iii) Ufugaji wa ng'ombe, mbuzi, kondoo na kuku

(iv) Uchimbaji wa madini, hususani dhahabu - wachimbaji wadogo wadogo

(v) Biashara za aina mbalimbali

KILIMO, UVUVI na UFUGAJI ni AJIRA KUU za Jimboni mwetu - tuendelee kuboresha mazingira na vitendea kazi vyake.

Picha za hapa zinaonesha:
ziara ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo kijijini Kabegi, Kata ya Ifulifu.

Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Musoma Vijijini
www.musomavijijini.or.tz

P. O. Box 6
Musoma

Tarehe:
Jumatano, 3.4.2024