WANAVIJIJI WASHIRIKIANA NA SERIKALI KUJENGA KITUO CHA AFYA CHA KATA YA BUGWEMA

baadhi ya MAJENGO yanayojengwa kwenye Mradi wa kupanua ZAHANATI ya KIJIJI cha Masinono kuwa KITUO cha AFYA cha KATA ya Bugwema.

Na: Fedson Masawa
Msaidizi wa Mbunge
Alhamisi, 26.11.2020
Jimbo la Musoma Vijijini
SERIKALI imetoa TSH MILIONI 400 kupanua ZAHANATI ya Kijiji cha MASINONO iwe KITUO cha AFYA cha Kata ya BUGWEMA.
Kata ya BUGWEMA inaundwa na Vijiji vinne (4) ambavyo ni: Bugwema, Kinyang’erere, Masinono na Muhoji.  Vijiji vyote hivi vinatumia ZAHANATI moja (1) tu ya Kijijini Masinono.
UPANUZI WA ZAHANATI KUWA KITUO CHA AFYA
Michango ya ujenzi inatolewa na:
*SERIKALI:
Tsh Milioni 400 – SHUKRANI nyingi sana zinatolewa kwa Serikali yetu.
*WANAVIJIJI:
Wanavijiji kutoka Vijiji vyote 4 na Viongozi wao wa Vijiji na Vitongoji wanachangia NGUVUKAZI zao kwa kusomba mawe, kokoto, mchanga na maji. Vilevile, wanachangia FEDHA taslimu.
*VIONGOZI wa KATA:
Diwani Mteule, Mhe Clifford Machumu na Diwani aliyemaliza muda wake, Mhe Ernest Maghembe wanaendelea kuchangia FEDHA taslimu na USAFIRI kwenye ujenzi huu.
*MBUNGE WA JIMBO:
Mbunge wa Jimbo, Prof Sospeter Muhongo, amechangia leo SARUJI MIFUKO 100  bado ataongezea Saruji Mifuko 300 kukamilisha AHADI yake.
MICHANGO mingine  ya Mbunge wa Jimbo kwenye ZAHANATI ya Masonono ni kama ifuatavyo:
(i) Gari 1 la Wagonjwa (Ambulance).
(ii) Nondo, Wavu na Masinki kwa ajili ya ukarabati wa choo cha Zahanati ya Masinono
MSIMAMIZI MKUU wa Mradi huu, Injinia Mrisho Shomari amesema, hadi sasa Mradi huo umetekelezwa kwa Asilimia 75 (75%) na kufikia mwishoni mwa mwezi Disemba, 2020  ujenzi utakuwa umekamilika kwa Asilimia 100 (100%).
Injinia Mrisho ametaja majengo ya KITUO hiki cha AFYA kuwa ni:
(i) Wodi ya Mama na Mtoto
(ii) Maabara
(iii) Jengo la Upasuaji
(iv) Jengo la Kufulia
(v) Jengo la Maiti (mortuary)
(vi) Vyoo vya nje, na
(vii) Miundombinu ya kutolea uchafu.
MGANGA MFAWIDHI wa Zahanati ya Masinono, Ndugu Mzalendo Wambura amewaomba WADAU wa MAENDELEO wakiwemo WAZALIWA wa KATA ya BUGWEMA kuwaunga mkono Wananchi wa Kata ya Bugwema na Serikali ili kukamilisha Mradi huu mapema iwezekanavyo.
MIUNDOMBINU YA HUDUMA ZA AFYA NDANI YA JIMBO LA MUSOMA VIJIJINI
*Zahanati 24 za Serikali
*Zahanati 4 za Binafsi
*Zahanati Mpya 14 zinajengwa
*Vituo vya Afya 2
(Murangi & Mugango)
*Hospitali ya Wilaya inajengwa Kijijini Suguti
*VITENDO KWANZA
*MAENDELEO KWANZA
Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Musoma Vijijini