MKUU WA WILAYA AENDELEA NA ZIARA YA KIKAZI MUSOMA VIJIJINI

 

Mkuu wa wilaya ya Musoma Dkt. Vicent Naano Anney (kulia) akikaribishwa kuzungumza kwenye mkutano uliofanyika kwenye kijiji cha Bukima.

Na. Verdiana Mgoma

MKUU wa wilaya ya Musoma Dkt. Vicent Naano Anney ameendelea na ziara yake ya kuzunguka kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo na kusikiliza kero za wananchi wake.

Akiwa katika Jimbo la Musoma Vijijini, Dkt. Naano alifanya ziara katika kata ya Bwasi na Bukima na kufanya mikutano ya hadhara kusikiliza kero zinazowakabili wananchi wa kata hizo ikiwemo changamoto za elimu, maji, mradi wa kilimo cha umwagiliaji (Nyakanda) ambao umesimama na haufanyi kazi

Akijibu kero hizo Dkt. Naano kwanza aliwashukuru wananchi hao kwa kuungana na serikali kuhakikisha wanapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya vyumba vya madarasa hasa kwa msaada mkubwa kutoka kwa Mbunge wa jimbo hilo Prof. Sospeter Muhongo ambao umefanikisha ujenzi wa vyumba saba na kuviezeka.

Mkuu huyo wa wilaya aliahidi kushirikiana na wananchi hao na Mbunge wao katika kuhakikisha ujenzi wa vyumba vya madarasa vilivyosalia na maabara kwenye kata hiyo vinakamilika mapema.

“Kwa juhudi mnazoendelea kuonyesha kwa kuipa elimu kipaumbele katika kata yenu, nitaungana nanyi na mheshimiwa Mbunge kuhakikisha tatizo la vyumba vya madarasa linakwisha kabisa” alisema Dkt. Naano.

Kwa upande wa sekta ya afya, mkuu huyo wa wilaya aliwataka wakazi wa eneo husika kutoa ushirikiano zaidi katika kutimiza malengo yao hasa kwa upande wa ujenzi wa kituo cha afya cha Bukima ili kuboresha zaidi huduma za afya kwenye kata hiyo.

Mbali na hayo, Dkt. Naano amewataka wakazi wa eneo hilo kujikita zaidi katika kilimo hasa cha umwagiliaji kutokana na kuwepo kwa miradi ya kilimo na fursa ya upatikanaji wa maji kwa urahisi, hivyo amewataka kulima zaidi mazao ya nafaka.