WAZEE WA MUSOMA VIJIJINI WAUNDA BARAZA LAO

Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wazee kutoka kwenye vijiji mbalimbali ndani ya jimbo lake ambao walikutana kwenye kijiji cha Murangi na kuunda baraza ambalo litafanya shughuli za kijamii ndani ya jimbo hilo.

Na. Mwandishi Wetu

WAWAKILISHI wa wazee wa vijiji 68 vya Jimbo la Musoma vijijini wamekutana na kuunda baraza lao ili kurahisisha na kuboresha mawasiliano baina ya wazee na jamii inayowazunguka.

Malengo mengine ya kuanzishwa kwa baraza hilo ni  kuweka pamoja mawazo ya wazee katika kusimamia maadili ndani ya jamii na kuishauri serikali katika suala zima la utekelezaji na ufuatiliaji wa shughuli za maendeleo.

Kikao hicho cha wazee hao kilichofanyika Januari, 23, katika kijiji cha Murangi, kilihudhuriwa na mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo, madiwani na mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Musoma pamoja na wazee wawili kutoka katika kila kijiji walio wawakilisha wazee wenzao kutoka vijijini.

Wakizungumzia muundo wa baraza hilo, wazee wa Jimbo la Musoma vijijini wamekubaliana kuwa, muundo wa baraza hilo uanzie ngazi ya kijiji, kata hadi jimbo ambapo kila muundo utakuwa na wajumbe wake watakaochaguliwa na wazee wenyewe kutoka kila ngazi husika.

Aidha, wazee hao wamemshukuru Mbunge wao Prof. Sospeter Muhongo kwa ubunifu wake na kwa kuwajali wazee na wananchi wote wa Jimbo la Musoma vijijini.

Wakati huo huo, Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Muhongo alitumia fursa hiyo kugawa kwa uwazi milioni 26 fedha za mfuko wa jimbo ambapo jumla ya shule 15 zimenufaika na mgao huo.

Shule hizo zimetengewa fedha hizo za kununulia mabati 54 kwa kila shule kwa ajili ya kuezeka chumba kimoja cha darasa katika harakati za kupunguza uhaba wa vyumba vya madarasa kwenye shule za msingi na sekondari ndani ya jimbo la Musoma vijijini.

Shule zilizonufaika na mgao huo kwa upande wa shule za msingi ni Nyegina, Kambarage, Mugango, Chanyauru B, Tegeruka, Rusoli, Busekera, Butata, Bugoji, Kamatondo, Kusenyi B na Kanyega, huku shule za sekondari ni Busamba, Bulinga na Mabui.