UVCCM MUSOMA WATAKIWA KUTUMIA VIZURI FURSA ZA MAENDELEO

Wasaidizi wa Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini James Francis (kulia) Verdiana Mgoma na Hamisa Gamba wakifuatilia Kikao cha Baraza la Umoja wa Vijana wa CCM ( UVCCM) kilichofanyika kwenye kijiji cha Suguti.  

Na. Verdiana Mgoma

UMOJA wa Vijana wa CCM (UVCCM) Wilaya ya Musoma umefanya kikao chake kwenye Kijiji cha Suguti na kujadili masuala mbalimbali ya kiuchumi na maendeleo.

Akizungumza kwenye kikao hicho Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Mara Jacob Mangalaya alisema, Jumuiya hiyo inapaswa kuachana na utegemezi na ili kufikia malengo hayo wanatakiwa kuunda vikundi vitakavyo wanufaisha kiuchumi, kijamii na kisiasa kulingana na fursa zilizopo.

Mwenyekiti huyo alisema, vikundi vitakavyoundwa vinatakiwa kupewa elimu ya kutosha, huku akisisitizia wajumbe kujitokeza kwenye suala la michezo na kugusia zoezi la uhakiki wa mali za UVCCM.

Kwa upande wake Katibu wa UVCCM Wilaya ya Musoma Joseph Mbogo alielezea jinsi ambavyo mfuko wa vijana ulivyowasaidia kuwapa mikopo na kuwawezesha katika miradi ya kilimo, uvuvi na urandaji mbao.

Katibu huyo alisema, mbali na mafanikio hayo waliyoyapata kutokana na mikopo, wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika utendaji wa kazi zao za kila siku ikiwemo kukosa usafiri, sare na kadi kwa wanachama wapya pamoja na upungufu wa vitendea kazi kwa watendaji ngazi ya kata na wilaya.

Hata hivyo, alimshukuru Mbunge wa Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa juhudi na mchango wake kwenye chama na maendeleo ya jimbo kwa ujumla.