ZAIDI YA MILIONI 100 YAPATIKANA KWENYE ZOEZI LA KUCHANGIA ELIMU

Mkuu wa wilaya ya Musoma Dkt. Vicent Anney akizungumzia miradi ya ujenzi wa maabara na vyumba vya madarasa kwenye kikao alichoshirikisha madiwani, wenyeviti pamoja na watendaji wa kijiji cha Chumwi.

Na. Verdiana Mgoma

WANANCHI wa vijiji mbalimbali vya Jimbo la Musoma vijijini wanaendelea kuitikia wito wa Mkuu wa Wilaya Dkt. Vicent Anney aliyewataka kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa na maabara ambapo zaidi ya shilingi milioni 100 imepatikana.

Dkt. Anney alitoa wito huo mapema mwezi Mei, mwaka huu na kuelekeza kila kaya katika Halmashauri ya Musoma vijijini kutoa mchango wa shilingi 15,000 kwa ajili ya ujenzi huo.

Maelekezo hayo yalipelekwa kwenye vikao vya ngazi ya vijiji na kata na kupata ridhaa ya wananchi ambao walikubaliana kuchangisha kila mwananchi mwenye umri zaidi ya miaka 18 na vijiji vingine vimekubaliana kuchangisha kaya kama ilivyoelekezwa.

Hivi sasa michango hiyo inaendelea kukusanywa kwa vijiji vyote 68 na kusimamiwa na serikali za vijiji, ingawa kasi ya uchangiaji hairidhishi, mpaka sasa fedha iliyokusanywa ni shilingi 108,539,900 ikilinganishwa na kiasi cha fedha kilichokisiwa kukusanywa shilingi 520,710,000 kwa makadirio ya fedha hizo ni sawa na asilimia 21 tu ya fedha iliyo kusanywa.

Kwa maelekezo yaliyotolewa hadi kufikia tarehe 31, Disemba, 2017 halmashauri ikamilishe ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha kwanza.

Kutokana na changamoto hiyo, halmashauri iliandaa kikao kilichojumuisha watendaji na viongozi wa halmashauri ili kutatua changamoto na kuunga nguvu kwa ajili ya kazi iliyo mbele ya ujenzi wa vyumba vya madarasa na maabara.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Musoma vijijini Dkt. Mgema Rutema, akitoa taarifa ya mahitaji ya madarasa na maabara kwa shule za msingi na sekondari alisema, shule za msingi zina upungufu wa vyumba 8,00 vya madarasa, shule za sekondari zina upungufu wa vyumba 56 vya madarasa na vyumba 40 vya maabara.

“Kutokana na mapungufu hayo, malengo tuliyojiwekea ni  kuhakikisha kuwa vyumba vyote vinakamilika ifikapo tarehe 8, Januari, 2018 siku ambayo shule zitafunguliwa” alisema Rutema.

Aidha, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa Mkuu wa wilaya juu ya hamasa ya uchangishaji wa mchango wa shilingi 15,000 kwa kaya na shilingi 10,000 ni kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na shilingi 5,000 kwa ajili ya ujenzi wa maabara.

Kupitia michango hiyo, kuna baadhi ya vijiji vilivyo hamasika na kufanya vizuri zaidi katika ukusanyaji, vijiji hivyo ni Murangi, Busekera, Busamba, Kwikuba, Buira, Bukumi, Kome, Buranga, na Butata, huku vijiji vinavyotajwa kuwa na kasi ndogo ni Mhoji , Mayani, Nyabaengere, Kiriba, Kakisheri, Kinyang’erere na Buanga.

Kupitia kikao kilichofanywa na halmashauri, kwa lengo la  kujifunza kwa waliofanikisha zoezi la uchangishaji, kupata msaada wa uzoefu na mbinu zinazotumika ili iwepo fursa ya viongozi wa vijiji ambavyo zoezi la uchangiaji linasuasua, kuona namna ya kutoa msaada hasa katika uhamasishaji.

Katika kikao hicho, baadhi ya sababu zilizo tajwa kupunguza kasi ya uchangiaji ni pamoja na baadhi ya viongozi wa vijiji kutofafanua vizuri lengo la michango hiyo kwenye mikutano yao, kuingizwa siasa katika michango hiyo ambapo wanasiasa wamekuwa wakiwaambia wananchi kwamba hakuna haja ya kuchangia kwasababu elimu ni bure.

Sababu nyingine zinazotajwa kuteteresha zoezi hilo ni historia ya michango ya nyuma ambayo mapato na matumizi hayajasomwa, hivyo wananchi kuingiwa na wasi wasi wa kupoteza fedha zao na nyingine ni kutokuwepo kwa stakabadhi halali za serikali kwa ajili ya uchangishaji, watendaji kutosimamia ukusanyaji wa michango na baadhi ya vijiji kutokuwa na watendaji.

Hata hivyo, ipo mikakati ya kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa ambapo imeundwa tume kwa ajili ya kusimamia kazi hiyo na kuongeza nguvu kwenye timu za ukusanyaji ngazi za vijiji na kata kwa kubuni mifumo na utaratibu ili kuhakikisha kila kaya inatoa mchango na kusimamia matumizi yake na kuandaliwa mfumo wa ukusanyaji wa fedha kwa kutumia stakabadhi halali za serikali.

Akizungumza katika kikao hicho Mkuu wa wilaya Dkt. Vicent Anney alisema, changamoto walizonazo ni nyingi katika idara ya elimu, lakini malengo yaliyopo ni kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa na maabara na kuwataka viongozi wa kata na vijiji kusimamia shughuli za maendeleo ili kuboresha elimu.

Dkt. Anney alisema, sababu zilizotolewa na baadhi ya viongozi juu ya fedha wanazochangisha kama changamoto ya kutofikia malengo hayo, isiwe visingizio vya wao kukwamisha michango na kuwataka kufanya kazi za maendeleo kwa bidii.

Mkuu huyo wa Wilaya alisema, ofisi yake itatoa ushirikino kwa viongozi na wananchi ili kuwezesha miradi hiyo yote na kukamilika kwa wakati, huku akiwataka kufikia Januari, 2, 2019 wahitimishe zoezi la uchangishaji, na matumizi ya michango iliyo kwisha kuchangishwa yatajadiliwa kupitia vikao vya WDC, tayari kwa ujenzi wa vyumba vya madarasa na maabara.