KIJIJI CHA SARAGANA WAONGEZA CHANZO KIPYA CHA MAPATO

Baadhi ya akinamama wa kijiji cha Saragana waliojitolea kushiriki kwenye zoezi la ujenzi wa choo cha eneo la mnada wakiwa na ndoo za kuchotea mchanga kwa ajili ya ujenzi huo.

Na. Hamisa Gamba

WANANCHI wa kijiji cha Saragana wameanza rasmi shughuli za ujenzi wa choo katika eneo la mnada ulioko kijijini hapo.

Lengo la kujengwa kwa choo hicho mbali na kuzuia magonjwa ya mlipuko kutokana na eneo hilo kukutanisha idadi kubwa ya watu, pia una lengo la kuingiza mapato kwa serikali ya kijiji.

Kabla ya ujenzi huo, eneo hilo halikuwa na huduma hiyo baada ya choo cha awali ukuta wake kuanguka na paa kuezuliwa na upepo mkali.

Uamuzi wa kuanza ujenzi huo ulichukuliwa kwenye kikao cha wananchi hao na serikali ya kijiji ambapo walisomewa mapato na matumizi na ikabainika kijiji hicho hakina vyanzo vya kutosha vya mapato zaidi ya malipo ya minara ya simu na uchinjaji wa ng’ombe.

Kwenye kikao hicho Mwenyekiti wa kijiji cha Saragana, Leni Manyama baada ya mtendaji wa kijiji Silivey Adam kusoma taarifa ya mapato na matumizi, aliwaomba wananchi kuchangia kuchangia nguvu kazi zao ili kukamilisha ujenzi huo ambao utasaidia kuongeza mapato ya kijiji.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri Frola Yongolo aliweka msisitizo kwenye kauli ya mwenyekiti huyo na kuwataka wananchi kushiriki kwenye ujenzi huo ambao iwapo utakamilika utasaidia kuongeza mapato ya kijiji na hata kusaidia kupambana na magonjwa.

Hata hivyo, wananchi hao walipokea suala hilo na kuanza mara moja utekelezaji, ingawa waliomba Halmashauri iwasaidie maji kutokana na ukame wakati huu wa kiangazi.