KIKAO CHA ‘WARD C’ CHATOA TAMKO UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAENDELEO BUKIMA

Wajumbe wa kikao cha Ward C wakiwemo wataalamu na wazee mashuhuri waliokaribishwa kwenye kikao hicho, wakifuatilia kwa makini mijadala mbalimbali iliyokuwa ikiendelea ndani ya kikao hicho.

Na. Mwandishi Wetu

KIKAO cha Ward C Bukima kimetoa agizo kwa viongozi wa kijiji cha Bukima pamoja na vijiji vingine vya kata hiyo kuhakikisha miradi mbalimbali ya maendeleo katika vijiji hivyo inatekelezwa na kukamilika kwa wakati.

Maamuzi hayo yamechukuliwa ili kuwapa moyo wafadhili mbalimbali wanaotoa michango yao akiwemo Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ambaye ametoa mifuko ya saruji, mabati na hata vitabu vinavyohitaji maktaba kwa shule zote za sekondari na msingi.

Tamko hilo limetolewa katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa ofisi ya Kata ya Bukima na kuhudhuriwa na wajumbe wa Ward C, wataalamu mbalimbali pamoja na wazee mashuhuri wa kata ya Bukima, ambapo ajenda 12 zilijadiliwa ikiwemo “Tathimini ya Mipango ya Maendeleo Ndani ya Nusu Mwaka kwa Vijiji vitatu vya Kata ya Bukima” ambavyo ni Bukima, Butata na Kastam.

Katibu wa kikao hicho ambaye pia ni Mtendaji wa kata ya Bukima Peter Magesa alisema, kati ya vijiji vitatu vya kata ya Bukima; Bukima, Butata na Kastam, ni vijiji viwili peke yake ambavyo vimefanikiwa kukamilisha mipango yao kwa kipindi chote hicho cha nusu mwaka.

Magesa alisema, Kijiji cha Bukima ambacho kimebaki nyuma kwa kila kitu hali ya kuwa fedha za kutekeleza miradi wanazo na ni kijiji chenye uwezo mkubwa ukilinganisha na vijiji vingine.

Alisema tayari kijiji cha Kastam kimekamilisha ujenzi wa vyumba vinne na ofisi na tayari kati ya hivyo, vyumba viwili vimekwisha kuezekwa kwa msaada wa Mbunge (chumba kimoja na ofisi) na Halmashauri chumba kimoja.

Aidha, kijiji cha Butata tayari wamekamilisha ujenzi wa vyumba viwili kwa msaada wa mifuko 60 ya saruji iliyotolewa na Mbunge, huku Bukima pamoja na kufyatua matofali, lakini bado wanasuasua katika utekelezaji wa ujenzi wa vyumba vya madarasa na wodi ya akinamama na watoto katika zahanati ya Bukima.

Wajumbe wa kikao hicho kupitia kwa Karebu Masuluri, waliwataka viongozi wa kijiji cha Bukima kuweka wazi matatizo na changamoto zinazowafanya wasitekeleze mipango hiyo ya maendeleo kwa wakati kabla ya kikao kutoa maamuzi na ushauri dhidi ya viongozi wa serikali ya kijiji cha Bukima.

“Kwanza tupate maoni kutoka kwa viongozi wakuu wa eneo husika ili waweze kutueleza matatizo yanayowasibu, kisha nasi tuweze kupata sehemu ya kusaidia. Tukiangalia hata kwa hali ya kawaida kijiji cha Bukima ni kijiji tajiri kuliko vijiji vingine vya kata ya Bukima na kina matajiri wanaoweza kuchangia michango yao. Tuwaombe viongozi watuelezee Mheshimiwa Mwenyekiti” alisema na kuomba Masuluri.

Akieleza changamoto zinazowakabili na kushindwa kutekeleza, kukamilisha miradi hiyo kwa wakati, Mwenyekiti wa kijiji cha Bukima Murungu Murungu alisema ni wajumbe wa serikali wengi wao kuwa na itikadi za kivyama, kuwepo na makundi kwa wenyeviti wa vitongoji pamoja na baadhi ya wajumbe kutohudhuria vikao vya serikali ya kijiji tangu wachaguliwe na kuapishwa, hivyo kubakia kuwa wakosoaji na wakwamishaji wakuu wa maendeleo na kutofautiana katika maamuzi ya kimaendeleo.

Wajumbe wa kikao hicho cha Ward C Bukima chini ya Mwenyekiti wa kikao hicho January Simula (diwani wa kata ya Bukima) baada ya kumsikiliza mwenyekiti wa kijiji hicho, waliagiza serikali ya kijiji cha Bukima kukaa chini ili kumaliza tofauti zao na kufikia 24, Julai mwakahuu tayari wawe wamekwisha kujenga na kutekeleza miradi hiyo kwa kasi na kamati itapita kukagua hatua itakayokuwa imefikiwa.

“Suala hili tumelijadili sana kwenye vikao kuanzia vikao vyao vya serikali ya kijiji, lakini tunaona ni kama tunaumiza vichwa bila mabadiliko yoyote sasa chakufanya sisi kama wajumbe wa kikao hiki cha Ward C, tunawapa muda kufikia Julai 24, 2017, tunahitaji kukuta kazi imekwishafanyika na ikamilike kwa wakati. Hatutaki tena porojo wala stori. Kinyume na utekelezaji wote mtawajibishwa kwa mujibu wa taratibu za kisheria” aliagiza na kusisitiza Simula.

Hata hivyo baadhi ya wajumbe walipendekeza kuwa, ikiwezekana katibu wa kikao awaandikie barua viongozi wote wa vyama vilivyowaweka madarakani wawajadili na kuwashauri wawajibike katika majukumu yao ikishindikana basi vyama vyao vichukue hatua kali dhidi yao au kushitakiwa kwa mujibu wa taratibu za nchi.