PROF. MUHONGO ATOA FUTARI KWA WAUMINI WA KIISLAMU JIMBONI KWAKE

Msaidizi wa Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini, Ramadhan Juma akihakiki baadhi ya vyakula vya futari vilivyotolewa na Prof. Sospeter Muhongo kwa ajili ya waumini wa kiislamu Jimboni kwake.

Na. Mwandishi Wetu

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ameungana na waislamu wa jimboni kwake kwa kuwapa futari katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan.

Akizungumza na waumini wa kiislamu wakati wa zoezi la usambazaji wa chakula hicho, Msaidizi wa mbunge Ramadhan Juma amewaeleza waumini hao kuwa, Prof. Muhongo yupo pamoja na amewataka kuiombea nchi amani katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan.

Akifafanua kuhusu mgawanyo wa chakula hicho, msaidizi huyo amesema, vyakula vilivyotolewa na mbunge ni mchele (kilo 930), maharage (kilo 475), sukari (kilo 350), mafuta (lita 195) na tambi (Katoni 35).

Vyakula hivyo vimegawanywa kwenye misikiti 36 iliyopo katika jimbo la Musoma vijijini na mgawanyo huo umezingatia idadi ya waumini katika kila msikiti.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa upokeaji wa chakula hicho, waumini hao wamemshukuru mbunge wao kwa jinsi anavyowajali bila kuangalia itikadi ya dini.

“Hakika huyu kiongozi ni mwema, yeye ni mkristo lakini anawajali hadi waislamu na kuutambua huu mwezi mtukufu, Mwenyezi Mungu amzidishie na ampe afya njema” alisema kiongozi wa msikiti wa Montah al-qalaf (Nyakatende) ustaadh Mzidalifa Ayub.

Naye kiongozi wa msikiti wa Taq’wa (Rukuba) Shekhe Mzamiru Yahya alimshukuru Prof. Muhongo kwa jinsi anavyowajali wananchi wa jimbo lake.

“Kwa mara ya kwanza nilimwona akija hapa Rukuba kukabidhi madawati kwa shule yetu ya msingi, akaleta saruji na mabati kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, na sasa amegeukia upande wa kugawa futari, hakika huyu amefunuliwa na Mungu ili awaokoe watu wake. Daima Mungu yuko pamoja nae” alisisitiza Shekhe Yahya.

Kwa upande wake, Shekhe wa Wilaya, Shekhe Bakari Ekonjo alibainisha kuwa, Waislamu hawana la kusema juu ya mbunge tofauti na kumshukuru na kumwombea maisha marefu na yenye Baraka tele.

Pia amesema, majaribu anayoyapata ni mipango ya Mungu na Mungu ndiye atamwonyesha njia ya kutokea,  alimwomba msaidizi wake kuwa, siku moja mheshimiwa mbunge afike jimboni kwa ajili kumwombea dua.

“Tufikishie salamu zetu kwa Mheshimiwa, hakika huyu ndo nabii wetu kwa watu wa Musoma vijijini na Mkoa wa Mara kwa ujumla, aliyokwishayafanya ni picha tosha kwa watanzania wote. Mungu atamwinua daima” alimalizia Shekhe Bakari.