SHULE ZA MSINGI JIMBO LA MUSOMA VIJIJINI KUBORESHA MAKTABA ZAKE

Untitled

Moja ya maktaba zinazopatikana kwenye shule za msingi za jimbo la Musoma vijijini ambazo zipo kwenye mkakati wa kuboreshwa.

Na Fedson Masawa

SHULE za msingi zenye maktaba katika jimbo la Musoma vijijini zimeahidi kuboresha maktaba zao ili kuziweka katika mazingira mazuri zaidi ya kujisomea watoto pamoja na wananchi wenye uhitaji wa kujisomea kutoka nje ya shule hizo.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Burungu, Mkama Ng’aranga, alisema shule yake ina mpango wa kupanua maktaba hiyo ili kutoa fursa kwa wanafunzi wengi kuingia na kujisomea.

“Shule yangu ina mpango wa kupanua maktaba hii ili kutoa fursa kwa watoto kutoka shule nyingine na wananchi wa kawaida kuingia na kujisomea bila shida yoyote. Pia utaratibu huu utakuwa ni kivutio kwa vijana wa vijijini kuja kujisomea na niombe walimu wenzangu wakilifanya hili basi tutakuwa mfano wa kuigwa” alisema Mwalimu Ng’aranga.

Akizungumzia umuhimu wa kuwepo kwa maktaba bora, Mwalimu Paschal Aloyce ambaye ni msimamizi mkuu wa taaluma shuleni hapo, alisema maktaba hiyo itatoa hamasa kwa wanafunzi wa shule hiyo kwani mazingira bora ya wanafunzi kujisomea ni njia moja wapo ya kuwa na ufaulu bora katika shule, hivyo basi kuwa na maktaba kubwa na bora ni kuongeza ufaulu bora kwa wanafunzi wao.

“Maktaba bora shuleni ndio ufaulu bora wa wanafunzi. Kuwa na maktaba bora hapa shuleni naamini kabisa vijana watajituma na hawatotumia muda wao mwingi kuzurura mitaani. Hivyo matokeo yao yatakuwa mazuri zaidi” alieleza mwalimu Aloyce.

Aidha, Magreti Trutumbi ambaye ni mwanafunzi wa darasa la saba shuleni hapo, ametoa shukrani zake za dhati kwa viongozi wa serikali na shule kwa kuwajengea maktaba na kujaza vitabu kwani haikuwa hali ya kawaida kwa wao kupata eneo sahihi la kujisomea na sasa wamelipata.

Kwa upande wake Filimon Elifath alishukuru kwa mchango mkubwa anaotoa Mbunge wao Prof. Muhongo ikiwa ni pamoja na vitabu, madawati, mifuko ya saruji na mabati kwa ajili ya kufanikisha mazingira bora ya taaluma yao katika shule zote za jimbo lao.

“Tunamshukuru mbunge wetu Prof. Muhongo kwa mchango wa mabati, saruji na vitabu anavyotupa. Itatusaidia katika kufaulu masomo yetu. Nasisi wanafunzi tunaahidi kufanya vizuri zaidi kwenye mtihani wetu wa mwisho” alishukuru na kuahidi Filimon.