WANAVIJIJI WANAENDELEA NA UJENZI WA ZAHANATI ZA VIJIJI VYAO

Wanavijiji wa Jimbo la Musoma Vijijini wanaendelea na ujenzi wa zahanati za vijiji vyao kwa kushirikiana na Madiwani wao, na Mbunge wao wa Jimbo.

Jimbo la Musoma Vijijini lina Kata 21 zenye vijiji 68 na vitongoji 374. Kila kijiji kimedhamiria kujenga zahanati yake.

Utaratibu unaotumika ni huu hapa:
(i) Wanakijiji wanabuni mradi wa ujenzi wa zahanati ya kijiji chao, wanatayarisha eneo la ujenzi, na wanapewa ushauri kutoka kwa Mhandisi wa Halmashauri yetu (Musoma DC)
(ii) Mbunge wa Jimbo, Prof Sospeter Muhongo anapiga Harambee ya kuanza ujenzi wa zahanati ya kijiji husika
(iii) Mbunge huyo anaendelea kushirikiana na wanakijiji kuchangia ujenzi wa zahanati inayojengwa hadi hapo Serikali itakapoanza kuchangia ukamilishaji wake.
(iv) Serikali hukamilisha ujenzi wa zahanati na kuweka vifaa tiba na wafanyakazi wanaohitajika.

Jimbo letu lina jumla ya Zahanati 29 zinazotoa Huduma za Afya. Kati ya hizo, 25 ni za Serikali na 4 ni za Binafsi.

Jimbo lina Vituo vya Afya sita (6) na Hospitali moja (1) ya Halmashauri/Wilaya.

Zahanati 16 zinaendelea kujengwa:
Vijiji vinavyojenga zahanati mpya ni hivi vifuatavyo: Burungu, Butata, Chanyauru, Chimati, Chirorwe, Kaburabura, Kakisheri, Kataryo, Kurukerege, Kurwaki, Kwikerege, Maneke, Mabuimerafuru, Nyabaengere, Nyambono na Nyasaungu.

Ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Kataryo:
Kijiji cha Kataryo ni moja ya vijiji vitatu vya Kata ya Tegeruka. Vijiji vingine ni: Mayani na Tegeruka. Kata hii inayo zahanati moja tu inayohudumia vijiji vyote, na imejengwa Kijijini Mayani

Kijiji cha Kataryo kimeamua kujenga zahanati yake kwa kutumia nguvukazi na michango ya fedha za wanakijiji, na baadhi ya wadau wa maendeleo wa kijiji hicho.

Diwani wa Kata hiyo, Mhe Alpha Modikae Mashauri amechangia Saruji Mifuko 50, na amehaidi kuendelea kuchangia ujenzi huo.

Mbunge wa Jimbo ameanza kutoa michango yake, kwa kuanza na Saruji Mifuko 200, nae ataendelea kuchangia ujenzi huo.

Akaunti ya Benki ya Kijiji cha Kataryo:
Benki: NMB
Akaunti Na: 30302300302
Jina la Akaunti: Kijiji cha Kataryo

Wana-Kataryo wanaomba mchango wako uwasaidie kukamilisha ujenzi wa zahanati yao kabla ya Disemba 2024. Tafadhali tuma mchango wako wa fedha kwenye Akaunti ya kijiji chao.

Picha zilizoambatanishwa hapa zinaonesha:
Hatua iliyofikiwa kwenye ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Kataryo, Kata ya Tegeruka.

Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Musoma Vijijini
www.musomavijijini.or.tz

P. O. Box 6
Musoma

Tarehe:
Jumatatu, 3.6.2024