KAMPENI YA SENSA MUSOMA VIJIJINI – KATA YA MAKOJO WAHAIDI KUHESABIWA KWA KIWANGO CHA ASILI MIA MOJA

Hatua kubwa iliyofikiwa kwenye ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Makojo.

Kata ya Makojo ina Vijiji 3 (Chimati, Chitare na Makojo) imemhaidi Mbunge wao wa Jimbo, Prof Sospeter Muhongo, kwamba wamejitayarisha kuhesabiwa wote, yaani kwa kiwango cha asili mia moja (100%)

Hiyo ahadi ilitolewa siku ya Jumamosi, tarehe 13.8.2022 wakati Mbunge huyo alipokuwa ndani ya Kata hiyo akifanya kampeni ya kushawishi Wanavijiji wa Kata hiyo (na Wageni wao) washiriki kwenye SENSA ya Watu na Makazi ya tarehe 23.8.2022.

Wakati wa majadiliano ya umuhimu wa kila kaya na kila mwananchi kuhesabiwa, Mbunge huyo aliwakumbusha Wana-Kata hiyo VIPAUMBELE vya MAENDELEO ya KATA yao (k.m. Elimu, Afya, Kilimo, Uvuvi) vinavyohitaji ushiriki na uchangiaji mkubwa wa Serikali yetu.

Viongozi wa Kata hiyo waliofuata na Mbunge wa Jimbo kwenye Kampeni hii ni:
*Ndugu Peresi Mujaya
(Mtendaji Kata, WEO)
*Ndugu Lameck Mtaki
(Mtendaji wa Kijiji, VEO)
*Ndugu Daniel Magere
(M/K Serikali ya Kijiji)

Miradi mikubwa ya Kata hii iliyokwishapata au inaendelea kupewa fedha kutoka Serikalini ni ifuatayo:

Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Makojo

Kata imeishapokea Tsh Milioni 500 (Tsh 500m) kutoka Serikalini kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya.

Wanavijiji na Viongozi wao wanaishukuru sana Serikali kwa kuwapatia Mradi huu muhimu sana. Shukrani za kipekee ziende kwa Mhe Rais Samia Suluhu Hassan.

Mradi wa Maji ya Bomba ya Ziwa Victoria

Mradi huu wa thamani ya Tsh bilioni 1.072 (Tsh 1, 072m) ni wa kusambaza maji ya bomba kwenye Vijiji vya Chitare na Makojo.

Mradi ulianza kwenye Mwaka wa Fedha 2013/2014, ulisimamiwa na Halmashauri yetu na umechelewa kukamilika.

RUWASA inajitahidi kurekebisha kasoro zilizopo.

Wananchi wana imani kubwa na Serikali yetu ambayo itahakikisha Mradi huu unakamilika na maji safi na salama yanapatikana ndani ya Kata ya Makojo.

Fedha za UVIKO- 19

*Makojo Sekondari ilipewa Tsh Milioni 60 (Tsh 60m) kujenga vyumba vipya 3 vya madarasa

*Shule Shikizi Mwikoko ilipewa Tsh Milioni 60 (Tsh 60m) kujenga vyumba vipya 3 vya madarasa na Ofisi 1. Shule hii tayari ilishapewa fedha za ujenzi wa vyumba vipya 2 vya madarasa na Ofisi 1 kutoka Mradi wa Serikali wa EQUIP.

Fedha za Mfuko wa Jimbo

*Makojo Sekondari imegawiwa Mabati 158 na Saruji Mifuko 52 kutoka kwenye Fedha za Mfuko wa Jimbo zilizonunua (Mei 2022) vifaa vya ujenzi kwa Sekondari kadhaa za Jimboni mwetu.

Miradi ya TARURA ndani ya Kata ya Makojo

*TARURA imekamilisha na inaendelea kuboresha barabara za eneo hili:

*Barabara ya Makojo- Chitare – Kurugee

*Barabara ya Chitare- Mwikoko Rusoli

Barabara hizi ni muhimu sana kwa uimarikaji wa uchumi wa wavuvi na wakulima wa eneo hili.

BAADHI YA MIRADI MIPYA ILIYOPANGWA KUTEKELEZWA NDANI YA KATA YA MAKOJO

(1) Uvuvi wa Vizimba – wavuvi wako tayari kuanzisha vyama vya ushirika vya uvuvi kwa lengo la kupatiwa mikopo ya uvuvi wa vizimba

(2) Ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Chimati unaendelea.

(3) Makojo High School – Wanavijiji wamemuomba Mbunge wao ashirikiane nao kwenye ujenzi wa “High school” hiyo – Mbunge amekubali ombi hilo na kikao cha mradi huo kitafanyika mwishoni mwa Septemba 2022.

UMUHIMU MKUBWA WA KUHESAMBIWA

Wanavijiji wa Kata ya Makojo wanao uelewa mkubwa wa umuhimu wa kuhesabiwa – wanakubali kwamba takwimu sahihi zinahitajika kwa mipango mizuri ya miradi yao ya maendeleo.

Kwa hiyo, Kata ya Makojo, kama zilivyo Kata nyingine 20 za Jimbo la Musoma Vijijini, WATAHESABIWA WOTE, yaani kwa asili mia moja (100%)

Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Musoma Vijijini
www.musomavijijini.or.tz

Tarehe:
Jumanne, 16.8.2022